May 16, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Polisi Arusha wapanda miti 1,700, kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi

Na. Mwandishi wetu Jeshi la Polisi

Jeshi la Polisi Mkoa wa Arusha limepanda zaidi ya miti 1,700 katika kambi ya kikosi cha Kutuliza Ghasia iliyopo maeneo ya Morombo jijini Arusha kwa ajili ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

Akiongoza zoezi hilo la upandaji miti Machi 13, 2024 Mkuu wa Operesheni za Polisi mkoani humo Kamishna Msaidizi wa Polisi ACP Salvas Makweli amesema jeshi hilo limelazimika kupanda miti hiyo kuunga juhudi za Serikali katika kukabiliana na hali ya ukame inayosababishwa na mabadiliko ya tabianchi.

Aidha ametoa wito kwa wananchi mkoani humo, kupanda miti katika maeneo yao ili kutunza mazingira kukabiliana mabadiliko hayo ya hewa huku akitaja faida za miti zikiwa ni pamoja na kuondoa jangwa, kupata sehemu za mapumziko pamoja kuzuia mmomonyoko wa ardhi.

Naye Koplo Sheila Mwakaleja ametoa wito kwa Askari wenzake kuwa na utaratibu wa kupanda miti katika maeneo yao wanayoishi ili kutunza mazingira na kuufanya Mkoa huo kuwa na hali ya hewa nzuri.