May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Ndejembi:Serikali yatenga sh.300 bil uboreshaji wa shule tisa

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma

NAIBU Waziri wa Nchi,Ofisi ya Rais ,Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Deo Ndejembi amesema,Serikali inatarajia kupata fedha kiasi cha shilingi bilioni 300 ambazo zinakwenda kuboresha miundombinu katika shule tisa za sekondari za Ufundi za Serikali zinazotarajiwa kufufuliwa.

Ndejembi ameyasema hayo leo Mei 14 jijini Dodoma wakati akifunga kongamano la Kitaifa la la Sera na Mitaala lililofanyika jijini humo kwa muda wa siku tatu.

Amesema,lengo ni kuhakikisha wakati shule hizo zinapoanza kuchukua wanafunzi zinatakiwa kuwa zimeboreshwa miundombinu yake pamoja na kuwa na vifaa vya kujifunzia na kufundishia ili kupata vijana mahiri watakaohitimu katika shule hizo.

Hata hivyo amesema,kutokana na shule hizo kutotosha kuchukua wanafunzi wengi zaidi,Serikali itajenga shule za ufundi wa Amali  katika halmashauri ambazo hazina vyuo vya VETA ili kupata nafasi ya kuchukua wanafunzi wengi zaidi shule ambazo wanafunzi wakihitimu masomo watapata vyeti kama vinavyotolewa na VETA.

“Ni mpango wa Serikali wa kujenga chuo cha VETA katika kila halmashauri ambayo ilikosa chuo hicho,na kwa awamu ya kwanza tayari tumeshajenga katika halmashauri 63,kwa hiyo sasa shule hizi za ufundi zitajengwa katika maeneo ambayo VETA haijajengwa.”amesema Ndejembi na kuongeza kuwa

“Haya ni mageuzi na mabadiliko makubwa  sana,wadau wa elimu tunapaswa tutoe sapoti  kubwa sana kwa Wizara ya Elimu ili mageuzi yaweze kutokea hapa nchini katika sekta ya elimu.”

Awali Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia Prof.Adolf Mkenda aliwahakikishia wadau kuwa maoni yote waliyoyatoa yatachukuliwa na kwenda kfanyiwa kazi.

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia Prof.Caroline Nombo amesema,lengo la Kongamano hilo limefikiwa huku akiwapongeza wadau kwa kutoa maoni mengi yenye mashiko na maslahi mapana kwa Taifa.

Wakitoa maoni yao baadhi ya wadau wameiomba Serikali katika lengo la ke la kufufua shule za Sekondari za Ufundi  ,mtaala uzingatie na shule za sekondari za binafsi zenye mafunzo hayo ya Amali.

Aidha kwa upande wa lugha ya kufundishia wadau hao walishauri itumike lugha ya Kiswahili huku wakitaka kutumika kwa lugha ya kingereza kwa ajili ya kufundishia kuanzia darasa la awali mpaka vyuo vya kati.

Mwalimu Zabron Nzale kutoka kundi la Wakuu wa shule za sekondari Tanzania (TAHOSA) alisema,matumizi ya lugha ya kingereza kuwa kama lugha ya kufundishia yataondoa matabaka baina ya watoto wa shule za serikali na binfasi.

“Hili sisi tumeona linawezekana hata kwa shule za serikali,maana kama kwa shule za binafsi imewezekana,basi hata kwa shule za serikali inawezekana kabisa kingereza kikatumika kama lugha ya kufundishia,lakini pia tuongeze na lugha nyingine kama kispanyola na Kireno.”amesema Nzale