Na Judith Ferdinand,TimesMajira Online,Mwanza
IMEELEZWA kuwa matumizi ya mfumo mpya wa ulipaji wa Kodi ya Majengo (NaPA) pamoja na mfumo wa ulipaji ada za maegesho ya magari, yanatarajiwa kuimarisha uwajibikaji,ufuatiliaji wa mapato na matumizi ya mifumo ya kidijitali katika Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela mkoani Mwanza.
Hatua hiyo pia inatarajiwa kusaidia Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela kuongeza ufanisi katika ukusanyaji wa mapato pamoja na uwezo wa kutekeleza miradi na huduma za maendeleo kwa wananchi.

Hayo yameelezwa Septemba 8,2026 wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo Watendaji wa Kata na Mitaa wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela, yaliyolenga kuhakikisha watendaji hao wanauelewa mfumo huo na kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi, hususan katika kutambua na kusajili majengo yanayopatikana katika maeneo yao.
Akifungua mafunzo hayo Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela,Ummy Wayayu amesema,mbali na iKodi ya Majengo, mafunzo hayo yanahusisha pia moduli mpya kuhusu kodi ya maegesho huku matumizi ya mifumo hiyo yatasaidia kuongeza ufanisi katika ukusanyaji wa mapato ya halmashauri hiyo.
Wayayu amesema,halmshauri hiyo inatumia mawakala katika baadhi ya shughuli za ukusanyaji wa mapato, hivyo mafunzo hayo yatawajengea uwezo watendaji wa kufuatilia na kusimamia utendaji wa mawakala hao katika maeneo yao.
“Baada ya mafunzo haya tutaenda kuufanyia kazi mfumo huu ili kuhakikisha mapato yanakusanywa,mkatimize wajibu wenu na pasiwepo mtu wa kuwa na sababu yoyote, kwani nyenzo na vitendea kazi vyote mnavyo.Mkawasimamie na kuwapa ushirikiano mzuri mawakala ili kurahisisha zoezi la ukusanyaji wa mapato,”amesema Wayayu.

Kwa upande wa Mtendaji wa Mtaa wa Igalagala Sadick Haruna amesema,mafunzo hayo ni muhimu kwao kwa kuwa yatawaongezea ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.
Huku Mtendaji wa Mtaa wa Butuja Zakhia Dogan amesema,mafunzo hayo pia yatawasaidia kuondokana na changamoto zilizokuwa zikiwakabili awali hasa katika usajili wa majengo na ukusanyaji wa kodi za majengo hayo.


More Stories
Serikali:Usimamizi madhubuti wapunguza udanganyifu mitihani
Vyama vya Siasa vyatakiwa kuwa Mabalozi wa Bima
Wasusi Gongolamboto wanufaika na loyalty program