May 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mwili wa Askofu mstaafu kanisa la Anglikana Dayosisi ya Victoria Nyanza, wazikwa jijini Mwanza

Na Judith Ferdinand, TimesMajira Online, Mwanza

Miezi 732 sawa na miaka 61 ya maisha ya Askofu mstaafu wa kanisa la Anglikana Dayosisi ya Victoria Nyanza Boniphace Kwangu imefika tamati baada ya kuzikwa Desemba 5,2022.

Ambapo mwili wa marehemu huyo ambaye aliyekuwa Askofu mstaafu wa kanisa hilo,umezikwa katika kanisa la Anglikana Dayosisi ya Victoria Nyanza,lililopo jijini Mwanza.

Hii ni baada ya mwili wa Askofu huyo mstaafu kuonekana ukielea ndani ya maji katika Ziwa Victoria jirani na linapojengwa daraja la JPM,Desemba mosi,2022 majira ya saa 10:00 jioni katika kijiji cha Kigongo, Kata ya Idetemya Wilaya ya Misungwi.

Kufuatia tukio hilo Desemba 2,2022 akizungumza na waandishi wa habari mkoani hapa,Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza Wilbroad Mutafungwa,alieleza kuwa Novemba 28,2022 majira ya asubuhi huko Shibula Wilaya ya Ilemela Askofu mstaafu Boniphace Kwangu aliaga familia yake na kuelekea wilaya ya Sengerema kwa ajili ya kupokea malipo ya mwisho ya milioni 2 .5(2,500,000).

Baada ya kuwa ameuza eneo lake pamoja na nyumba kwa kanisa la KKKT- Sengerema,hata hivyo hakuweza kulipwa kiasi hicho cha fedha kwa kuwa wanunuzi walimtaka awasilishe nyaraka ya umiliki wa eneo hilo hivyo, alirudi Mwanza mjini kwa ajili ya kushughulikia nyaraka hizo.

Kamanda Mutafungwa alieleza kuwa ilipofika jioni ya siku hiyo familia yake walipata wasiwasi kuhusu alipo BoniphaceKwangu kwani alikuwa hajarudi nyumbani pia alikuwa hapatikani kwenye simu yake ya mkononi.

Kutokana na hali hiyo ilibidi familiayake watoe taarifa kituo cha Polisi Kirumba hivyo Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza kwa kushirikiana na familia na watu mbalimbali lilianza kufanya ufuatiliaji ili kubaini alipo askofu huyo mstaafu.

Akizungumza wakati wa ibada ya mazishi ya Askofu mstaafu Boniphace Kwangu,Askofu Mkuu wa Kanisa la Anglikana Tanzania, Mahimbo Mndolwa ameiomba Serikali na vyombo vya dola kufanya uchunguzi kufuatia kifo cha Askofu Mstaafu huyo ambacho kimetokea kwa njia ya kutatanisha.

Ameeleza kuwa imani yao kwa Jeshi la Polisi na serikali ni kuwa itafanyia kazi jambo hilo ili haki itendeke kwano hawatarajii kuona taifa lenye wahalifu na waovu wa kuweza kuondoa uhai wa mtu mwingine.

“Imani yetu kama kuna watu waliohusika kuondoa maisha ya baba huyu kwa namna moja ama nyingine Mungu anawajua na tunaamini vyombo vyetu vya ulinzi siku zote vimekuwa makini katika utendaji haki,litaifanyia jambo hili haki,” ameeleza Askofu Mahimbo.

Aidha amemshukuru serikali na Jeshi hilo kwa namna ambavyo wameshirikiana nao na mwisho wameweza kuwaruhusu kuulaza mwili wa marehemu huyo ambaye alikuwa Askofu mstaafu wa kanisa hilo tangu walipo toa taarifa ya kupotea kwake na hatimaye mwili wake kupatikana.

“Sisi hatuna mkono wa kufika mbali,sisi hatuna macho ya kuona mbali,sisi hatuna mkono wa kushika mtu muovu,lakini nyie mnao mkono huo tunawaombe hili kama kuna yoyote aliye husika kwa namna mmoja ama nyingine haki ya mtu ipatikane na familia ipate amani,tupate kusamehe kama kuna mtu aliye husika na kumjua tutamleta kwa Mungu na mengine tutaiachia serikali,”.

Akisoma historia ya marehemu ndugu wa marehemu,Benedicto Kwangu ameeleza kuwa pamoja na wito wa kumtumikia Mungu, Askofu huyo Mstaafu amewahi kuwa mwalimu wa somo la Fizikia na hesabu katika shule ya sekondari ya Mwanza na ameacha mjane na watoto watatu.

Pia ameeleza kuwa tukio hilo kwao ni la kwanza ingawa wanaamini katika kusamehe na kutendewa hakiAskofu wa kanisa hilo, Dayosisi ya Kagera, Darlington Bendankeha,ameekeza kuwa kuna watu wengine wanaoishi kama kwamba wataishi milele na kusahau kama na wao wameubwa kwa udongo.

Ameeleza kuwa wanadamu lazima wajifunze kuhesabu siku wanazoishi duniani kwa kuwa maisha ni mafupi hivyo wanatakiwa kuishi kwa kufuata kanuni mbili muhimu za kumpenda Mungu na kumpenda jirani kama nafasi yao.

Alieleza kuwa kuna watu wanaigiza kuwa wanampenda Mungu, lakini hakuna kitu kumbe ni waingizaji na hawana upendeo badala yake wamejaa unafiki na wanadanganya.

”Siku tunaishi kwenye dunia ambayo mauaji ni kitu cha kawaidi, kuna mauaji na ukatili mkubwa ndani ya jamii zetu mtu haogopi kumchinja mwenzake kwa ajili ya kupata utajiri, hatujui nani kesho atafuata na kwamba ili kuishi kwa kuhesabu siku, lazima mtu ujenge nguvu ya imani.”

Mtoto wa marehemu, Diogracius Ngwira akizungumza na waandishi wa habari baada ya maziko ya baba yake, alieleza kuwa walipata mshituko mara baada ya kutoweka nyumbani kwao Novemba 28 mwaka huu.Ameeleza kuwa baada ya baba yao kutoweka nyumba waliingia katika maombi kwani ni tukio la kwanza kutokea ndani ya familia yao.

“Baada ya kutoweka nyumba kwetu, baba yangu aliokotwa akiwa anaelea ndani ya maji katika eneo la Bukumbi Ziwa Victoria,kama alivyosema Askofu Mkuu tunaamini katika msamaha na haki na wale waliopewa jukumu la kusimamia wafanye hivyo na sisi tunaamini katika msamaha mara nyingi hatusamehi kwa sababu ya tunayemsamehe bali tunasamehe kwa ajili yetu sisi,” ameeleza.

Askofu Mkuu wa Kanisa la Anglikana Tanzania, Mahimbo Mndolwa,akifanya sala katika jeneza lenye mwili wa marehemu Askofu mstaafu wa kanisa hilo Dayosisi ya Victoria Nyanza Boniphace Kwangu,katika ibada ya mazishi iliofanyika katika kanisa hilo jijini Mwanza.
Baadhi ya waumini waliohudhuria ibada ya kumuaga aliyekuwa Askofu mstaafu wa kanisa la Anglikana Dayosisi ya Victoria Nyanza,iliofanyika katika kanisa hilo jijini Mwanza.