May 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mwenyekiti Act -Wazalendo apokelewa Zanzibar rasmi

Na Mwandishi wetu,timesmajira

Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo Taifa ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Othman Masoud Othman, amerejea nyumbani Zanzibar akitokea katika Ziara Maalum ya Kichama, Jijini Dar es Salaam.

Othman ambaye ameambatana na Safu yote ya Viongozi Wakuu ambao walichaguliwa hivi karibuni kupitia Mkutano Mkuu wa Taifa wa Chama ACT-Wazalendo, uliofanyika Machi 05 na 06 Mwaka huu, wamepokelewa kwa Matembezi Maalum kuanzia Bandari ya Malindi hadi ilipo Ofisi Kuu ya Chama hicho Vuga, Mkoa wa Mjini Magharibi, Unguja.

Hafla hiyo ambayo Othman ameambatana na Mke wake, Mama Zainab Kombo Shaib, ililenga pia kuwatambulisha Viongozi wengine Wakuu wa Chama hicho, kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, ambao pia walipata fursa ya kusalimiana na umma wa Wananchi waliofika hapo kwaajili ya kuwapokea.

Waliohudhuria hapo ni pamoja na Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo Mkoa wa Dar es Salaam, Renatus Pamba, sambamba na Uwakilishi wa Viongozi na Wanachama kutoka Mikoa yote ya Unguja.

Mapokezi hayo yamepambambwa na hamasa ya aina yake, ikijumuisha pia Vikundi vya Burdani za Utamaduni, kutoka Mjini na Vijijini.