May 18, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Biliioni 9 kukuza ujuzi wa vijana 2024

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma

SERIKALI imesema,inatarajia kuanza programu ya kukuza ujuzi kwa vijana mwaka 2024 ambapo  kiasi cha shilingi bilioni 9 zimetengwa kwa ajili ya program hiyo.

Hayo yamesema na Waziri  wa Nchi ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Prof . Joyce Ndalichako wakati akizungumza kwenye mahafari ya 40 ya Chuo cha VETA Dodoma .

Prof.Ndalichako amesema kwa mwaka 2024,Programu imelenga kuwafikia vijana 6000 huku akisema lengo la programu hiyo ni kuwawezesha vijana kujiari na kujitegemea kiuchumi na hivyo kuchangia katika pato la Taifa.

“Serikali imetenga kiasi cha  shilingi  bilioni 9 kwa ajili ya program ya mafunzo na  kukuza ujuzi kwa vijana   6000 itakayoanza Januari  2024.”amesema Prof.Ndalichako

Amesema mafunzo ya ujuzi ni eneo la kipaumbele kwa serikali la kupunguza tatizo la ajira kwa vijana kwa kuwawezesha vijana waweze kujiajiri au kuajiriwa  na kuondokana na utegemezi kwa familia zao na taifa kwa ujumla.
Katika hatua nyingine Prof.Ndalichako amesema, kupitia mikopo inayotolewa kwenye ngazi za halmashauri serikali itaendelea kutoa kipaumbele kwa vijana ambao wamepata ujuzi.
Mkurugenzi Mkuu wa VETA  Dkt. Prosper Mgaya, amesema mafunzo ya Kukuza Ajira na Ujuzi (E4D) yameleta chachu ya kuleta maendeleo katika chuo hicho.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu ,Sayansi na Teknolojia ,Frenkly Rwezimula amekitaka VETA  kuanzisha program mbalimbali ambazo zitawafikia vijana wengi na zitakazolenga kuongeza thamani kwenye bidhaa mbalimbali

Naye Mshauri wa Mradi wa E4D ,Leah Dotto   amesema  mafanikio ya Mradi huo ni pamoja na  kuwafikia wanafunzi zaidi ya 40000 .