May 8, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza John Mongella kulia akiteta jambo na Mkurungezi Mkuu wa NHIF Bernard Konga,kwenye uzinduzi wa huduma za bima ya afya kwa Waandishi wa Habari nchini, uliofanyika mkoani Mwanza

Mpango huduma za bima ya afya kwa waandishi wazinduliwa Mwanza

Na Judith Ferdinand,TimesMajira Online, Mwanza

MPANGO wa huduma za bima ya afya kwa Waandishi wa Habari wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya(NHIF),umezinduliwa ambapo jumla ya wanahabari 65 na wategemezi wao 20 wakiwa wamejiunga.

Akizungumza wakati wa halfa ya uzinduzi wa mpango huo uliofanyika mkoani Mwanza,Mkuu wa Mkoa wa Mwanza John Mongella, amesema maendeleo yanaweza kuporomoka endapo kama afya itakuwa dhaifu,kwani afya ni mtaji mkubwa katika maisha ya binadamu na inaleta tija katika maisha binafsi,familia, taasisi na taifa kwa ujumla hivyo Waandishi wa Habari watumie fursa hiyo kujiunga na mpango huo wa bima ili kuwa na uhakika wa matibabu.

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza John Mongella (wa pili kushoto),akiwa ameshika kwa pamoja boksi lenye kadi za bima za afya za waandishi wa habari waliojiunga na mfuko huo,na Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt.Angeline Mabula(wa pili kulia) ambapo wa kwanza kushoto ni Mkurungezi Mkuu wa NHIF Bernard Konga na wa kwanza kulia Rais wa UTPC Degratius Nsokolo Picha zote na Judith Ferdinand

“Suala la afya ni nyeti sana katika muktada wa maendeleo ya taifa,wanahabari ni kundi linalo sahaulika sana na ni sekta muhimu sana hasa katika kipindi hiki,hivyo kupata bidhaa hi ambayo inamgusa moja kwa moja kupata huduma ya afya ni jambo jema ambalo limefanywa na NHIF,” amesema Mongella.

Hata hivyo aliwataka kutilia mkazo suala la kuelimisha jamiikuhusiana na umuhimu wa bima,pia amekuwa akiwaambia viongozi wenzake ni vyema wakatilia mkazo kuelimisha jamii kuhusiana na suala hilo ambalo ni muhimu kwa afya na maendeleo ya taifa.

Kwa upande wake Mkurungezi Mkuu wa NHIF Bernard Konga, amesema lengo la mpango huo ni kutoa suluhu kwa wanahabari katika kukabiliana na gharama za matibabu kwani wamekuwa wakishuhudia kundi hilo linavyopata shida pindi mmoja wao au mmoja wa wanafamilia anapougua wanavyohangaika kugharamia matibabu.

“Hii ni kutokana na ukweli kwamba kundi hili halikuwa na utaratibu maalum wa kuhudumiwa katika mfumo wa bima ya afya na hatimaye walikua wanajiunga wachache kupitia utaratibu wa kikoa,hivyo mfuko kwa kushirikiana na Umoja wa Klabu ya Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC) na Klabu za Waandishi za mikoa tukiendelea kuwa na mikutano ya elimu kwa waandishi katika mikoa na tukaona kuna haja kwa kundi hili kuwa na utaratibu wake wa kujiunga na mfuko huu,”amesema Konga.

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza John Mongella kulia akiteta jambo na Mkurungezi Mkuu wa NHIF Bernard Konga,kwenye uzinduzi wa huduma za bima ya afya kwa Waandishi wa Habari nchini, uliofanyika mkoani Mwanza.

Amesema,kwa takwimu walizopewa vyama vya waandishi wa habari nchini jumla vipo 28 vyenye jumla ya wanachama 1,800, ambapo hadi kufikia septemba 13,ni wanahabari 65 na wategemezi wao 20 wamejiunga,hivyo ameiomba UTPC kuchangamkia fursa hiyo kwa kuwakumbusha na kuhakikisha wanachama wao wajiunga na mfuko huo kabla ya kuugua ambao itamlazimu kuchangia 100,080.

Naye Naibu Waziri wa Ardhi,Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt.Angeline Mabula, amesema hakuna mwenye mawasiliano na Mungu kuwa lini ataugua na hatakua kuwa na fedha,lakini ukiwa na bima ya afya unakuwa umewekeza katika afya na kuwa na uhakika wa kupata matibabu hivyo Waandishi watumie fursa hiyo kujiunga pia wawe sehemu ya mabalozi wa kuhamasisha wananchi kujiunga na mfuko huo.

Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Mwanza (MPC) Edwin Soko akizungimza kwenye uzinduzi wa huduma za bima ya afya kwa Waandishi wa Habari nchini

Rais UTPC Deogratius Nsokolo,amesema kati ya klabu 28 zilizopo nchini ambao wanachama wake wamejiunga na mpango huo ni klabu 11 ikiwemo klabu ya mkoa wa Kigoma 17,Mwanza 16, Mbeya 11,Shinyanga 11, Zanzibar 8, Dodoma 5, Dare es salam 3, Rukwa 1, Simiyu 2, Katavi 2, huku akiziagiza Klabu kuendelea kuhamasisha waandishi wa habari kujiunga na vifurushi hivyo hata kwa kuchangia fedha kidokidogo.

Hata hivyo Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mwanza (MPC),Edwin Soko amesema mpango huo ni matokea ya kikao walichokaa wanachama wa MPC na NHIF mkoani hapo,hivyo aliahidi kusimamia ili kila mwanachama aweze kujiunga na bima hiyo.