May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mila,desturi bado kikwazo kwa wanawake kumiliki ardhi

Na Penina Malundo, timesmajira online

Licha ya kuwepo kwa sheria zinazoruhu wanawake nchini kumiliki ardhi lakini bado mila na desturi katika baadhi ya jamii zimekuwa kikwazo kwa wanawake kutumia haki yao kisheria katika ardhi kufanya shughuli mbalimbali ikiwemo kilimo na ufugaji.

Asilimia kubwa ya wanawake
wanaopata changamoto ya kushindwa kutumia haki yao kisheria ya kumiliki ardhi ni wale wanaoishi maeneo ya vijijini kwa sababu mila na desturi zilizopo katika jamii zao bado zinataka wanawake kuwa chini katika kumiliki ardhi licha ya sheria kuwa wazi.

Ibara ya 24(1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 (kama ilivyorejewa mara kwa mara) inaainisha ya kuwa kila mtu anayo haki ya kumiliki mali na haki ya
hifadhi ya mali yake aliyonayo kwa mujibu
wa sheria.

Huku sera ya taifa ya Ardhi ya mwaka
1995 na sheria za ardhi namba 4 na
5 ya mwaka 1999 ,nazo zinazosisitiza
juu ya haki sawa kwa mwanaume na
mwanamke katika kupata,kutumia na
kumiliki ardhi kama sehemu ambayo kila
raia wa Tanzania ana haki ya kumiliki kwa
mujibu wa katiba ya nchi.

Hivyo wanawake na wanaume wana
haki sawa katika kumiliki ardhi kama
mojawapo ya mali ambayo wamechuma
wote kwa pamoja na sio mwanaume
pekee ake ndio mwenye haki ya kumiliki
ardhi kama mila na desturi za baadhi ya
makabila zinazosema.

Kutokana na watu wengi kutojua sheria
za umiliki wa ardhi hivyo kuchangia ukatili
wa kijinsia kwa wanawake wengi, serikali
kwa kushirikiana na mashirika mbalimbali
ikiwemo Shirika la Wanawake katika
Maendeleo Barani Afrika (WiLDAF)
wamekuwa wakiongeza mwamko kwa
wanawake kujua sheria katika umiliki wa
ardhi na ushiriki katika maamuzi.

Mwanasheria wa Wildaf Zakia Msangi,
anasema kisheria haki ya kumiliki ardhi
kwa wanawake zinaboresha hali ya
usawa wa kijinsia,ulinzi wa kiuchumi na
hadhi ya kijamii,kwani wanapokosa haki
hizo wanawake wengi hukosa sauti za
kuzungumza katika vikao vya maamuzi.

Anasema sababu kuu zinazopelekea
kuvunjika kwa haki za wanawake katika
kumiliki ardhi ni pamoja na uwepo
wa sheria za kibaguzi,mila na desturi
mbovu,mitizamo hasi juu ya haki ya
wanawake kumiliki ardhi na kuwaona
wanawake wanaopigania haki zao
kuonekana watu wenye tamaa.

‘’Umiliki wa ardhi mara nyingi unakuwa
ni wa Mkuu wa Kaya ambaye ni baba
kama mila na desturi zinavyoonesha kwa
makabila mengi kwa nchi za Afrika,hii
inatokana na kuamini kuwa mwanaume
ndio sauti ya familia jambo ambalo sio
sahihi kisheria,’’anasema na kuongeza kuwa

‘’Katiba ya nchi inatambua umiliki halali
wa mali kwa mwanamke na mwanaume
na hakuna mahali pametengwa au
kuonesha kuwa mwanaume anaweza
akamiliki ardhi alafu mwanamke asiweze
kumiliki,’’anasema.

Anasema mila na desturi juu ya umiliki
wa ardhi inachangia kwa kiasi kikubwa
mwanamke kudidimizwa kifkra,kiuchumi
na hata kimaendeleo kwa kuonekana
kuwa hana uwezo wa kumiliki ardhi
kama aliokuwa nao mwanaume.

Hii ni kutokana na namna mwanamke anapofiwa na mumewe au kuachana kwenda
kuanzisha familia nyingine hivyo familia
kuhofia mali waliyotafuta na mwanaume
wake wa kwanza kupotelea kwa familia
nyingine.

Msangi anasema sheria ya ardhi na sheria ya vijiji zote nchini Tanzania zimetambua umiliki sawa wa mali kati ya mwanamke na wanaume.

’’Inapokuja suala la wanandoa mmeamua kuishi
pamoja na mali ya ardhi,mmeipata
pamoja ni mazoea tuliyokuwa nayo
sisi ya kuandika jina la baba pekee
ake kama kichwa cha familia na kama
yeye ndio mmiliki wa kiwanja lakini
sheria ipo vizuri na wazi inatambua
kuwa ardhi hiyo mnayonunua mnaweza
kumiliki pamoja na katika hati ya ardhi
inaweza kuandikwa jina la mume na
mke na hapo hapatakuwa na ugomvi
wowote,’’anasema na kuongeza kuwa

‘’Ikija suala la mgawano napo inakua
rahisi hata inapotokea kifo kwa mtu
mmoja wao kufariki ugawaji wa mirathi
inakuwa ni rahisi zaidi kuliko kuandika jina
la mtu mmoja,’’anasema.

Msangi anasema inapotokea mtu
anapewa mali kabla ya kufunga ndoa
na baba ake au mtu yoyote ambapo
anamiliki yeye kabla ya kuwa katika ndoa,
mali hiyo inakuwa yake binafsi ila kama
ulipatiwa mali hiyo mkiwa mmeishi muda
mrefu na mkaamua kuiendeleza itakuwa
imeingia katika ndoa.

WILDAF inavyopambania umiliki wa ardhi kwa wanawake

Msangi anasema wanachokifanya Wildaf
katika kupambana na ukatili huo wa kijinsia
ni kutumia sheria kama nyenzo
ya kuweza kumkomboa mwanamke
kiuchumi,kisiasa,kijamii,kisheria ikiwemo
katika suala la umiliki wa ardhi ambapo
wanawake wengi wamekuwa wakinyimwa
haki zao za ulimiliki wa ardhi.

Anasema hata inapotokea kwenye
mgawanyo wa mali hasa upande wa
mirathi,mwanamke anaonekana haki
yake ni kupata vyombo vya ndani na
baadhi ya mifugo kama kuku au bata
lakini inapokuja suala la ardhi au magari
vitu hivyo vinakuwa ni vya mwanaume.

‘’Hapo ndipo Wildaf tunapoingia na
kuwasaidia wanawake katika kuangalia
sheria inasemaje katika masuala ya
ardhi,kwani sheria ipo wazi inasema
mwanamke anaweza kumiliki ardhi sawa
na mwanaume endapo wamepata mali
hizo pamoja,’’anasisitiza.

Aidha anasema Wildaf inatoa msaada wa
kisheria bure kwa wanawake wanaopitia
ukatili wa kijinsia kama huo wakunyimwa
kumiliki ardhi,kiuchumi,kingono,kimwili
wanamsaidia kisheria katika kupinga
ukatili wanaokabiliana nao.

Kwa upande wake mmoja wa
wanawake jamii ya kimasai,Catherine
Losurutia,anasema kuna umuhimu
mkubwa wa mwanamke kumiliki ardhi
kwani yeye ndio mtu anaeangalia familia
na ndie anayejua matumizi sahihi ya ardhi
kama ni kufuga au kulima.

Anasema wanawake wanapaswa
kutoona ardhi inamilikiwa na wanaume
pekee yao na kukaa kimya bali wanapaswa
kupaza sauti katika mashirika ya kisheria
ili waweze kusaidika kutokanana na
baadhi ya jamii kuona mwamke hana haki
katika umilikiji wa ardhi.

‘’Unamuachia mwanaume amiliki ardhi
unakuja kushangaa imeshauzwa,mama
na watoto wanaanza kuangaika huku na
huko hivyo kuwafanya kukosa haki yao
ya msingi,’’anasema.

Losurutia anasema yeye kama
mchechemuzi amekuwa mstari wa
mbele kutoa elimu juu ya umuhimu wa
wanawake kumiliki ardhi na kuhakikisha
wanaweka wanaweza kumiliki rasilimali
hiyo ili iweze kuwasaidia katika shughuli
zao mbalimbali.