May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mikopo maendeleo ya jamii, wanufaika watoa kongole mbele ya katibu mkuu – Dkt Chaula

Na Mwandishi wetu, Timesmajira Online

Mikopo ya zaidi ya Milioni 170 iliyotolewa na Serikali kupitia Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum na kuwanufaisha Wajasiriamali kwenye  jiji la Dodoma imeonekana kufanya vizuri huku wahusika wakiipongeza Serikali kwa hatua hiyo.
 
Pongezi hizo zimetolewa na wanufaika hao kwa nyakati tofauti wakati wa ziara ya Menejimenti ya Wizara hiyo ikiongozwa na Katibu Mkuu wake Dkt. Zainab Chaula walipovitembelea vikundi hivyo Novemba11, 2022.
 
Aziza Abdi ambaye ni Mkurugenzi wa Kampuni inayojishughulisha na uchakataji wa taka za Plastiki ambaye alipokea Millioni 100 alisema anaipongeza sana Serikali kwa hatua hiyo ya kuwawezesha mikopo kupitia Wizara kwani imewawezesha kupanua biashara hiyo ambapo kwa sasa anauwezo wakuchakata tani 130 kwa mwezi tofauti na hapo awali walipoanza mwaka 2013 ambapo walikuwa wakizalisha tani 40 pekee.
 
“Mbali na kuongeza uzalishaji lakini kwa sasa nimenunua gari, moja nimefanikiwa kuongeza ajira kutoka 20 hadi 60 za kudumu sambamba na kuboresha maslahi yao lakini wafanyakazi wa kutwa wanafikia 300 kwa sasa” amesema Aziza.
 


Bi Yolanda Kaswalala anayejishughulisha na uchakataji wa bidhaa za Mlmazao ikiwepo uzalishaji wa mafuta ya Alizeti, usagaji unga wa Ukoboaji wa nafaka ambaye alipata mkopo wa millioni 50 amesema kwa sasa ameongeza mashine zake hivyo anaipongeza sana Serikali.

Kwa upande wa Kikundi cha Five Dadas wanaojishughulisha na uokaji wa mikate na bidhaa za ambao ni wanufaika wa mkopo wa Millioni 20 walisema wamefanikiwa kuonunua gari moja na pikipiki tatu zilizosaidia kuboresha biashara zao.
 
Akizungunza mara baada ya ziara hiyo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. Zainab Chaula amesema shabaha ya ziara hiyo ni kuachana na mambo ya nadharia na badala yake nadharia hizo zibadilike na kuwa kwenye vitendo.
 
“Ziara yetu hii tumekuja kuamsha ari na kuchochea morali kwa wanajamii wao wenyewe watumie rasilimali zinazo wazunguka ili waweze kuzibadilisha changamoto kuwa fursa” amesema Dkt. Chaula.


 
Dkt. Chaula ameongeza kuwa, imefika wakati kwa bidhaa zinazozalishwa na wajasiriamali wa ndani kufanyiwa utafiti na wanaokidhi vigezo wapatiwe alama za ubora, aidha akataka bidhaa zote ziwekewe alama itakayoitambulisha bidhaa husika na iwe vyepesi kutambulika kwenye mfumo wa ulipaji wa kodi ya Serikali kwenye mamlaka za serikali za Mitaa.
 
Akiongea wakati wa ziara hiyo, Mkurugenzi wa Maendeleo ya Jamii, Bw. Patrick Golwike  alisema Sera ya Maendeleo ya Jamii inawataka Maafisa Maendeleo ya Jamii kuamsha ari na kuleta uchechemuzi miongoni mwa jamii na kujiltea maendeleo kwa kutumia rasilimali zinazo wazunguka.