May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mifumo ya eGA inavyorahisisha utendaji kazi

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma

MAMLAKA ya Serikali Mtandao e-GA imetengeneza mifumo mipya kwa kutumia wataalam wake wa ndani ambapo mifumo hiyo imeshaanza kufanya kazi.

Lengo la mifumo hiyo ni kurahisisha utendaji kazi katika utumishi lakini pia kurahisisha upatikaji wa huduma kwa watumishi wa umma na wananchi kwa ujumla.

Akizungumza na waandishi wa habari katika maonyesho ya wiki ya Ubunifu jijini Dodoma, Afisa TEHAMA wa Mamlaka hiyo Tumaini Masinsi ametaja mifumo hiyo kuwa ni pamoja na  mfumo wa kuratibu shughuli za kimawasiliano kwa kupiga simu kwa Taasisi mbalimbali za Umma,Mfumo wa Akili bandia (ChatAI),Alphachain Blockchain Network na Sec Doc,eMrejesho,EBoard, Oxygen na RSS.

“Mfumo wa akili badndia ni ubunifu unaotumia teknolojia ya akili bandia kusaidia Mamlaka ya Serikali Mtandao kujibu maswali ya mara kwa mara kuhusiana na utendaji kazi wa Mamlaka, na Aphachain Blockchain Network ni ubunifu wa ndani unaohimiza matumizi ya mtandao wa blockchain kutengenza mifumo mbalimbali na Sec Doc  ni  ubunifu wa mtandao unaotokana na teknolojia ya blockchain yenye malengo ya kuongeza ulinzi kwenye matumizi na utumaji wa nyaraka mbalimbali.”amesema Masinzi na kuongeza kuwa

“eMrejesho mfumo wa kutuma, kupokea na kufuatilia malalamiko, mapendekezo, maulizo na pongezi kwenda kwa taasisi mbalimbali za umma ambapo eBoard ni  mfumo wa kuratibu vikao vya bodi na kamati zake, menejimenti na kamati zake pamoja na madiwani Mfumo huu umekua suluhu kubwa katika kupunguza gharama za utendaji kazi kwenye eneo hili la vikao.”

Aidha amefafanua kuwa “Oxygen ni ubunifu wa mtandao wa kijamii wenye usalama wa hali ya juu ulioundwa kwa lengo la kufanya mawasiliano kwa njia ya ujumbe mfupi  na RSS ni ubunifu wa teknolojia unaofanania na TeamView na Anydesk, unaruhusu ku share skrini za kompyuta kwa watu walio kwenye maeneo tofauti ya ki jiographia, pia unaruhusu utumaji na upokeaji wa ma faili mbali mbali kwa njia ya kielectroni.”

 Masinsi amesema kutokana na majukumu yao wanapaswa  kuhakikisha mifumo yote muhimu inatengenezwa na inafanya kazikwa lengo la  kuiunga mkono serikali katika jitihada za kuhakikisha sayansi,teknolojia na ubunifu vinatumika kwa faida na kuongeza uchumi wa Taifa.

Vanesa Mhando kutoka e-GA aamesema maonyesho hayo yanawatia moyo vijana kuendelea kufanya bunifu zinazoweza kutatua changamoto zilizopo katika jamii kwa kujenga mifumo ya kurahisisha utendaji kazi.