May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mhandisi Mahundi aunga mkono jitihada za Rais Samia kutangaza utalii wa ndani

Na Esther Macha,Timesmajira Online,Kyela

NAIBU Waziri wa Maji,Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Mbeya Mhandisi, Maryprisca Mahundi amemuunga mkono kwa vitendo Rais wa Samia Suluhu Hassan ya kutangaza na kuhamasisha utalii kwa kuwezesha wanawake zaidi ya 600 kutalii katika ufukwe wa Matema Ziwa Nyasa Wilaya ya Kyela.

Mhandisi Mahundi amesema hayo wakati alipokuwa kwenye fukwe za Ziwa Nyasa kwa lengo la kuunga mkono jitihada za Rais Samia za kutangaza utalii wa ndani (Royal Tour )pia kuwezesha kiuchumi wanawake.

Amesema kuwa amewaalika wanawake wa Mkoa wa Mbeya ili waweze kuunga mkono jitihada za Royar Tour na kwani Rais amefungua milango ambapo watalii wameanza kuja Tanzania zaidi wameweza kutembelea maeneo ya Nyanda za Kaskazini kwa maana ya hifadhi za wanyama na vivutio mbalimbali.

“Sisi wanawake wa Mkoa wa Mbeya tumuunge mkono Rais za kutangaza vivutio vyetu vilivyopo ndani ya mkoa wetu ambapo tumeanza na fukwe ya Ziwa Nyasa kwa hapa Kyela,pia tumefanya vikao vyetu vya kiuchumi,kisiasa na kijamii hivyo tumeweza kujiwekea mikakati yetu sababu sasa tunafunga mwaka na kuingia 2024 kwa hiyo ni mipango mipya namna ya kujikwamua kiuchumi “amesema Mhandisi Mahundi.

Mkuu wa Wilaya ya Kyela Josephine Manase amesema Ziwa Nyasa lina vivutio vingi wakiwemo samaki na dagaa hivyo wanakaribisha wawekezaji kwa ajili ya kusindika samaki na kufanya shughuli zingine na kusafirisha sehemu zingine.

“Ukiangalia samaki waliopo wengi wanatumika kwa Mbeya lakini tunahitaji mikoa mingine wawajue samaki hawa mbasa na dagaa wa Nyasa aina ya usipa ambao wana nyama nyingi tofauti na dagaa wengine tunakaribisha sana wawekezaji, “amesema Mkuu huyo wa Wilaya .

Issa Mwakasendo ni mmoja wa wananchi waliopata fursa ya kutembelea ufukwe wa Ziwa Nyasa amesema kitendo kilichofanywa na Mahundi kinapaswa kuigwa na viongozi wengine.

Baadhi ya vivutio vilivyopo katika Ziwa Nyasa ni pamoja na samaki ambao hawapatikani popote duniani na sanaa ya utengenezaji wa vyungu vya kupikia na mapambo.