April 27, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mfumo wa kielektroniki kuokoa maisha ya akina mama wajawazito na watoto wazinduliwa

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amezindua Mfumo wa Kitaifa wa usafirishaji wa dharura kwa akina mama wajawazito na wachanga m-mama huku akiziagiza Halmashauri zote zitakazopitiwa na mpango huo kutenga fedha kwa ajili ya kuusapoti na ulete tija iliyokusudiwa.

“Kama nilivyoagiza mwanzo kuhusu lishe bora kwa wajawazito na nikawataka watenge fedha na kusaini kuona matumizi ya fedha na lishe ya mama wajawazito inavyopanda ,leo nitawasiniasha wakuu wa mikoa hapa kuona kwamba mnatenga fedha zinazokwenda kusapoti kwengye mpango huo wa m -mama lengo likiwa ni kuokoa maisha ya mama wajawazito na watoto wachanga…,na ninaomba mkajipange vizuri katika kuufanyia kazi.”alisema Rais Samia

Akizindua mfumo huo uliotengenezwa na kampuni ya simu za mkononi Vodacom Tanzania,Rais Samia alisema, pamoja na mafanikio kadhaa yaliyopatikana hapa nchini bado wanawake na watoto wanapoteza maisha yao wakati wa kujifungua au muda mfupi baada ya kujifungua.

“Hali hii wakati mwingine inatokana na kukosekana kwa taarifa au mawasiliano ya haraka ya usafiri wa uhakika wa kuhakikisha kwamba mama mjamzito anafika kituo cha afya haraka na kupata huduma stahiki.”alisema

Uwekezaji wa Serikali kwa uhai wa mtoto unaonekana kupungua kwa vifo vya watoto kati ya mwaka 2010 na 2015 ambapo kiwango cha vifo vya watoto wachanga wenye siku 0-28 vimepungua kutoka vifo 40 hadi 28 kwa kila vizazi hai 1000,kiwango cha vifo vya watoto wachanga wenye umri wa siku 28 hadi miezi 11 vimepungua kutoka vifo 99 hadi 43 kwa kila vizazi hai 1000 na kiwango cha vifo vya watoto chini ya miaka mitano vimepungua kutoka vifo 147 hadi 67 kwa kila vizazi hai 1000.

Alisema,mfumo huo unakwenda kuwa suluhisho katika kupunguza kama siyo kuondoa kabisa vifo vya akina mama wajawazito waliopteza maisha kwa kukosekana usafiri wa haraka.

Vile vile ameielekeza  Wizara ya Habari ,Mawasiliano na Teknolojia ya habari kuhakikisha inakamilisha uandaaji wa sheria ya kulinda taarifa za watu binafsi ili taarifa za akina mama wanaohudumiwa kupitia mfumo huo zisambae mitandao mara baada ya kuhudumiwa.

Katika hatua nyingine Rais Samia ameilekeza Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) , Wizara ya Afya na wadau wengine kuhakikisha mfumo huo unakuwa endelevu na rahisi kwa mtumiaji ili uakisi malengo yaliyokusudiwa ya kuwafikia wananchi wengi zaidi.

Alisema uanzishwaji wa mfumo huo umesaidia pia kuunga mkono kampeni yake ya ‘jiongeze tuwavushe salama’yenye lengo la kuokoa maisha ya akina mama wajawazito na watoto wachanga.

“Sasa ni imani yangu kwamba mfumo huu tunaozundua leo umekwenda kujaribiwa na kuonyesha matokeo chanya katika kunusuru maisha ya mama mjamzito na mtoto wake kabla na baada ya kujifungua…,pia nimefurahi kusikia Wizara ya Afya wanafanyia kazi mfumo wa kufuatilia matumizi ya dawa tangu inaingia nchini mpaka inamfikia mgonjwa.”alisema Rais Samia na kuonmgeza kuwa 

Alisema,kwa upande wa Serikali iliahidi katika uboreshaji wa huduma za afya na kwamba imeanza na ujenzi wa miundombinu ambapo vituo kadhaa vimejengwa katika vijiji kata,wila na mikoa na hospitali za mikoa na kazi ya ujenzi inaendelea lakini kazi ya kununua na kuweka vifaa tiba katika vituo hivyo inaendelea huku kwa upande wa dawa akisema serikali imetoa fedha nyingi   kwa ajili ya dawa lakini pia  nimetoa agizo la kuiangalia Bohari ya Dawa haraka sana .

“Na hapa nimefurahi kusikia Waziri wa Afya akisema wanaandaa mfumo  wa kuifuata dawa mpaka inapoishia, naomba mfumo huu ufanyiwe kazi haraka sana  ili ulete tija kwenye enbeo hilo.”alisema na kuongeza kuwa

“Lakini pia serikali imejitahidi kuhakikisha maeneo yetu yanakuwa na ‘ambulance’ angalau kila kata ‘ambulance’’ moja,tumeagiza ‘ambulance’ 233 za kawaida ambazo zitaenda Tanzania nzima lakini pia tumeagiza ‘ambulance’ 25 ambazo ni ‘advance’ hizi ni kama kituo cha afya zina kila kitu , ,lakini pia tumeagiza magari 242 ya uratibu, ni matarajio yangu kwamba magari na ambulance yatakwenda kuongeza nguvu kwenye mpango huu wa m-mama .”

“Lakini kama haitoshi katika mwaka uliopita tumetoa fedha nyingi kwa Wakala wa Barabara za Mijini na Vijijini (TARURA) ili kujenga brabara za vijijini ziweze kupitika  misimu yote ili  paoja na shughuli nyingine lakini pia yaweze kupeleka wagonjwa harakaraka.”

Rais Samia ametumia nafasi hiyo kuyataka makampuni mengine yakiwemo ya simu za mkononi na yasiyo ya simu za mkononi kuiga mfano huo wa VODACOM kwa kuingia hata katika maeneo mengine siyo lazima iwe katika afya.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania Sitholizwe Mdlalose alisema,baada ya majaribio sasa mfumo huo unakwenda kutanuka kwenye mikoa 14 na tayari fedha zimeongezwa huku lengo likiwa ni kuwafikia  zaidi ya akina mama milioni moja katika mikoa hiyo 14.

Aidha alisema mradi ukiwa kwenye majaribio umeonyesha mafanikio makubwa ikiwa ni pamoja na  kupungua kwa vifo vya akina mama wajawazito wakati wa kujifungua  vinavyotokana na kukosekana kwa usafiri  wa haraka.

Naye Waziri wa Afya Ummy Mwalimu alisema kuwa Kutokana na kampeni aliyoibuni  Rais Samia  iliyokuwa inalenga kuwavusha salama kinamama wajawazito imeleta matunda kwani utendaji kazi wake umeonekana.

“Utendaji wa kazi yako katika kuhakikisha watanzania wanapata huduma Bora inaonekana,novemba 2017 ulibuni wewe mwenyewe na kuanzisha kampeni ya kitaifa ya jiongeze tuwavushe salama lengo ni kupunguza vifo vya  wakina mama wajawazito na watoto,

“Kazi yako imeleta matunda wakati

unazindua hiyo kinamama walipokuwa wanaohudhuria kliniki angalau mara nne katika kipindi cha ujauzito wao walikuwa ni asilimia 51,lakini leo wakinamama wanaohudhuria kliniki idadi yao imepanda hadi kufikia asilimia 65, mchango wako unaonekana wa kuokoa maisha kwa wakinamama wajawazito na watoto,”alisema Waziri Ummy

Alisema kuwa Wakati wa uzinduzi wa kampeni ya Jiongeze Tuwavushe salama’ wanawake walikuwa wanajifungulia zahanati katika zahanati na vituo vya afya ilikuwa ni asilimia 65 na sasa ni asilimia 81 huku lengo la Shirika la Afya Duniani (WHO)  linasema ifikie angalau asilimia 80 wanawake wajifungilie katika vituo vya afya hii inaonesha jitihada na juhudi za kuokoa maisha ya watanzania.

Alifafanua kuwa Sekta ya Afya chini ya awamu ya 6 inakwenda kuhesabu wakinamama wajawazito na watoto wakitanzania je wanapata huduma Bora za afya na si Bora huduma.

“Hatuta hesabu majengo tu tunajielekeza katika huduma Bora za afya na katika hili tumesema wakinamama asilimia 90 waweze kuhudhuria cliniki angalau mara 4 katika kipindi Cha ujauzo sasa hivi vifo vinatoka wapi hatutapenda kuona vifo vikiendelea kutokea kwa kina mama wajawazito wakati wa kujifungua,”alisisitiza.

Huku Waziri wa Habari Mawasiliano na Teknolojia ya habari Nape Nnauye alisema kuwa Serikali imekuwa ikifanya jitihada za makusudi za kutenga fedha kuwezesha utekelezaji wa miradi ya TEHAMA  ili kuchochea uzalishaji na utoaji huduma wa sekta nyingine ikiwemo sekta ya afya.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Maendeleo ya Jamii Stanlaus Nyongo alisema kampuni ya Vodacom wamefanya ubinifu mkubwa wa kuokoa maisha ya mama na mtoto huku akisema vifo kwa makundi hayo hakikubaliki.

Aidha alisema,mfumo huo pia unakwenda kusukuma Programu  Jumuishi ya Kitaifa ya Malezi,Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto kwa kuhakikisha mtoto anakuwa salama tangu akiwa tumboni kwa mama na baada ya kuzaliwa.

“Mfumo huu unashabihiana sana Programu Jumuishi ya Kitaifa ya Malezi,Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto,kwa hiyo tunaamini mama anaenda kuwa na uzazi salama lakini pia kuhakikisha usalama wa mtoto anayezaliwa kwa kufika haraka katika kituo cha afya kwa kutumia mfumo huo.”alisema Nyongo

Mmoja wa wazazi waliofika katika uzinduzi huo Mariam Juma alisema,kwa muda mrefu kumekuwa na changamoto ya vifo vya akina mama wajawazito  vinavyotokea kabla na baada ya kujifungua pamoja na vifo vya watoto wachanga vinavyotokea kwa sababu mbalimbali huku akisema ,sasa katika baadhi ya maeneo yenye changamoto za usafiri inakwenda kutatuliwa na hatimaye kuchangia katika kupunguza vifo vya akina mama na watoto wachanga.

Mradi huo ulianza kwa majaribio katika mkoa wa Shinyanga ambako baada ya kuonyesha tija sasa unakwenda kutekelezwa katika mikoa mingine 14 ambayo ni Morogoro,Tanga ,Pwani,Lindi,Tabora,Mtwara,Mara,Mwanza,Geita,Kigoma,Mbeya,Songwe,Rukwa na Dodoma.

Flora Kajumula ni Muuguzi Mkuu wa mkoa wa Shinyanga ambako mradi umetekelezwa kwa majaribio alisema,mfumo umeweza kupunguza vifo vya akina mama wajawazito kutoka 74 hadi 54 lakini pia imepunguza vifo vya watoto wachanga 1080 mpaka mwaka jana hadi vifo 665.