April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Maalim Seif awataka wanawake, vijana kugombea uongozi

Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online

CHAMA Cha ACT-Wazalendo Taifa kimewataka wanawake na vijana kujitokeza kwa wingi kuwania nafasi za uongozi kwenye Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 2020.

Wito huo umetolewa na Mwenyekiti wa chama hicho Taifa, Maalim Seif Sharif Hamad wakati alipokuwa akizungumza na wanachama wa ACT-Wazalendo ikiwa ni muendelezo wa ziara yake ya kuimarisha chama hicho kisiwani Pemba.

Amesema, wanawake na vijana wanamchango mkubwa katika kuleta mageuzi ya kisiasa na kiuchumi, hivyo endapo watajitokeza na kushinda kwenye wataweza kuwaletea maendeleo ya kweli wananchi wa Zanzibar.

“Taifa lolote duniani linahitaji wanawake na vijana ili kupiga hatua za kimaendeleo, nawaomba sana vijana wa kike na kiume mjitokeze kwa wingi kuwania nafasi mbali mbali za uongozi kwenye uchaguzi mkuu ujao na tumesema mara hii wanawake watakaowania kwenye majimbo na wakakosa lakini wakafanya kazi ya kugombea na wakakiletea chama asilimia 10 ya kura wagombea hao tutawapa kipaumbele katika viti maalum endapo watagombea” amesema.

Amesema, lengo la ACT-Wazalendo baada ya kushinda uchaguzi ni kuunda serikali shirikishi itakayojumuisha vijana na wazee wenye uzoefu ili kuleta ufanisi wa kiutendaji kwenye serikali watakayoiongoza.

Katika hatua nyengine Maalim Seif amewataka wagombea kuanzia ngazi ya urais, ubunge, uwakilishi na udiwani kutojihusisha na makundi yatakayoweza kule mgawanyiko ndani ya chama hicho, badala yake amewasisitiza kufanya siasa za kistaarabu zitakazoweza kuimarisha umoja.