May 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kampuni ya Twalib Yawashika mkono watoto yatima

Na Jackline Martin, TimesMajira Online

Kampuni ya Twalib inayojishughulisha na usafirishaji wa majini na anga, imetoa msaada wa vitu mbalimbali katika kituo cha kulelea watoto yatima ‘Alfurqaan’ chenye watoto wakiume 75 wenye umri wa miaka 3-18.

Vitu hivyo vilivyopelekwa katika kituo hicho kilichopo Chanika Jijini Dar es Salaam, ni pamoja na sukari, unga , mafuta ya kupaka, dawa za meno, sabuni za kufulia, chumvi, majani ya chai, n.k

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam, Meneja Masoko wa kampuni hiyo, Agnes Kalasan amesema kilichopelekea kwenda kutoa msaada katika kituo hicho ni kwasababu kinauhitaji wa vitu mbalimbali nikiwemo vyakula, magodoro, neti n.k

“Watoto hawa wanahitaji vitu vingi ikiwemo nguo, chakula, elimu n.k, hivyo tumeona si vyema kumaliza mfungo wa ramadhan bila kuja kuwaona watoto hawa na kuwaletea mahitaji mbalimbali”.

Kalashan alizisihi kampuni nyingine kujitoa kutembelea vituo mbalimbali vya kulelea watoto yatima ili kutatua changamoto walizonazo.

Naye Nasra Msofe kutoka taasisi ya jamii inayohusisha vijana, wanawake na jamii nzima – Tuamke pamoja Tanzania ameishukuru serikali kwa kutoa fursa ya elimu bure mashuleni katika ngazi ya sekondari lakini pia ameiomba serikali kuibua vipaji vya watoto hao yatima ili vipaji vyao visiishie njiani.

“Huwa tunatembea katika vituo mbalimbali kwa lengo la kwenda kuwasaidia watoto wenye uhitaji hasa watoto ambao hawana wazazi na wanaoishi katika mazingira magumu”

“Tunaiomba serikali iweze kuibua vipaji vya watoto viliivyopo kwenye vituo hivi ili waweze kujulikana na kusaidiwa zaidi”.

Naye Mfanyakazi katika kituo hicho, Jumanne Omary amesema ameanza kuishi na kuwalea watoto hao mwaka 2014 hivyo changamoto kubwa aliyokutana nayo kwa watoto hao ni elimu ambapo huwa wanauhitaji wa pesa za kufanyia mitihani mashuleni.

“Watoto hawa wanashindwa kufanya mitihani ya kumaliza shule kwasababu wanakosa pesa na kupelekea kukaa nje bila ya kufanya mitihani”

“Watoto hawa wapo 75, watoto 25 wapo sekondari na 50 wapo shule ya msingi na wote ni wakiume”.

Amelishukuru jeshi la Polisi la Chanika kwa kutoa ushirikiano wao katika kituo hicho ambapo kila baada ya miezi mitatu wanawatembelea na kuwapa elimu ya malezi ya watoto.

Mmoja wa watoto wanaolelewa katika kituo hiko, Japhar Chalamila amewashukuru Twalib kwa msaada walioutoa na kuwaomba watu wengine mbalimbali wazidi kuwatembelea ili kuendelea kutatua changamoto walizonazo ikiwemo ukosefu wa vitabu, mafuta na vyakula.