May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Gambo aimwagia sifa CRDB kwa ujenzi wa madarasa

Na Yusuph Mussa, TimesMajira Online, Arusha

MBUNGE wa Jimbo la Arusha Mjini Mrisho Gambo amesema Benki ya CRDB imekuwa ikitoa mchango mkubwa kwenye jamii kwa kurudisha faida wanayopata kwa kujenga miundombinu ya shule ikiwemo vyumba vya madarasa, madawati, vituo vya afya, zahanati na vifaa tiba.

Aliyasema hayo Mei 17, 2023 kwenye hafla ya Benki ya CRDB kukabidhi vyumba viwili vya madarasa kwenye Shule ya Sekondari Kalimaji, Kata ya Moshono, vilivyojengwa kwa ufadhili wa benki hiyo kwa gharama ya sh. milioni 42

“Benki ya CRDB imekuwa ni mtu mwema kwetu na kwa jamii ya Watanzania kwa kurudisha faida kwa wananchi. Wamefanya mambo mengi sio kwetu tu bali nchi nzima, kwani wamejenga kila mahali vyumba vya madarasa, madawati, vituo vya afya na mambo mengine.

“Hata hii shule hapa tulipo bila CRDB, leo tusingekuwa na shule hii. Wao ndiyo watu wa kwanza kujenga vyumba vya madarasa kwenye shule hiii. Ingekuwa hatuna uchoyo, shule hii tungeita CRDB Benki Sekondari School. Niseme, CRDB haina mpinzani, na kama yupo, basi ana kazi kubwa ya kufanya” alisema Gambo.

Gambo alisema wana mpango wa kujenga mabweni mawili kwenye shule hiyo iliyoanza masomo Januari, mwaka jana kwa gharama ya sh. milioni 150, ili kuwasaidia wanafunzi wanaotoka mbali, kwani hata kuanzishwa kwa shule hiyo, kulitokana na wanafunzi kutembea umbali wa kilomita sita kwenda shule.

Gambo alimuomba Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB Group Abdulmajid Nsekela kuwasaidia kununua kompyuta kwa wanafunzi wa shule hiyo.

Akizungumza na hadhara hiyo, Nsekela alikubali ombi la kuwanunulia kompyuta wanafunzi wa shule hiyo kwa kutoa sh. milioni 10, na kuongeza kuwa Benki ya CRDB ipo tayari kushirikiana na jamii na kuisaidia Serikali ya Awamu ya Sita ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwaletea wananchi maendeleo.

Mkuu wa Wilaya ya Arusha Felician Mtahengerwa ambaye alikwenda kwenye hafla hiyo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha John Mongella, alisema kwa kuwapatia vyumba viwili vya madarasa ni kwamba wanaunga mkono juhudi za Serikali, na wao wamekuwa ni Wazalendo kuona jamii inaneemeka kwa kuwepo benki hiyo hapa nchini.

“Kwa kutupatia haya madarasa, Benki ya CRDB ni Wazalendo, na wanamuunga mkono Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan. Pia wamesaidia Jiji la Arusha na kutatua mahitaji ya shule. Wenzetu Benki ya CRDB wametupa madarasa haya, hii ina maanisha tunapunguza msongamano wa wanafunzi kwenye shule na kuongeza ufanisi.

“Na hata walimu watapa utulivu kwenye kufundisha.. Niseme naguswa sana na Benki ya CRDB ilivyokuwa karibu na wananchi” alisema Mtahengerwa.

Mkuu wa Wilaya ya Arusha Felician Mtahengerwa (wa tano kushoto) akifungua kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha John Mongella, vyumba viwili vya madarasa kwenye Shule ya Sekondari Kalimaji iliyopo Kata ya Moshono vilivyojengwa kwa ufadhili wa Benki ya CRDB kwa gharama ya sh. milioni 42. Hafla hiyo ilifanyika Mei 17, 2023. Wengine ni Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini Mrisho Gambo (wa nne kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB Group Abdulmajid Nsekela (wa tano kulia), Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Foundation Tully Mwambapa (wa nne kulia), Meneja wa Benki ya CRDB Kanda ya Kaskazini Chiku Issa (wa tatu kulia). (Picha na Yusuph Mussa).
Mkuu wa Wilaya ya Arusha Felician Mtahengerwa akizungumza kwenye hafla ya Benki ya CRDB kukabidhi vyumba viwili vya madarasa Shule ya Sekondari Kalimaji, Kata ya Moshono vilivyojengwa kwa gharama ya sh. milioni 42 kwa ufadhili wa benki hiyo. Hafla hiyo ilifanyika shuleni hapo. (Picha na Yusuph Mussa).
Mbunge wa Arusha Mjini Mrisho Gambo
akizungumza kwenye hafla ya Benki ya CRDB kukabidhi vyumba viwili vya madarasa Shule ya Sekondari Kalimaji, Kata ya Moshono vilivyojengwa kwa gharama ya sh. milioni 42 kwa ufadhili wa benki hiyo. Hafla hiyo ilifanyika shuleni hapo. (Picha na Yusuph Mussa).
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB Group Abdulmajid Nsekela,
akizungumza kwenye hafla ya Benki ya CRDB kukabidhi vyumba viwili vya madarasa Shule ya Sekondari Kalimaji, Kata ya Moshono vilivyojengwa kwa gharama ya sh. milioni 42 kwa ufadhili wa benki hiyo. Hafla hiyo ilifanyika shuleni hapo Mei 17, 2023. Wengine ni Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Bank Foundation Tully Mwambapa (kulia) na Meneja wa Benki ya CRDB Kanda ya Kaskazini Chiku Issa (katikati). (Picha na Yusuph Mussa).
Vyumba viwili vya madarasa Shule ya Sekondari Kalimaji, iliyopo Kata ya Moshono katika Jiji la Arusha. Madarasa hayo yamejengwa kwa ufadhili wa Benki ya CRDB kwa gharama ya sh. milioni 42. Hafla ya kukabidhi madarasa hayo ilifanyika Mei 17, 2023. (Picha na Yusuph Mussa).