May 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

FCC yawakaribisha wawekezaji

Na Jackline Martin, TimesMajira Online

Tume ya ushindani FCC, imewaomba watu wote wanaokusudia kuja kuwekeza nchini kufika FCC wakiwa wamepata kampuni wanayotaka kuungana nayo kwani watahakikisha bidhaa zinazozalishwa na kampuni hizo wanazilinda na hakutakua na bidhaa bandia.

Hayo yalisemwa na Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC) William Erio wakati akizingumza na waandishi wa Habari Jana Jijini Dar es Salaam katika maonyesho ya 47 ya biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (SabasabaWawek).

“FCC tunahakikisha kwamba bidhaa bandia hazina nafasi nchini zisije kwa kuuzwa Wala kwa nia ya kama malighafi ya kuzalisha hapa nchini”

Aidha Erio alisema FCC wanashajihisha na kulinda ushindani, lengo ikiwa ni kuhakikisha kwamba katika shughuli za ushindani, wale ambao tayari wamefanya biashara wanafanya kwa kuzingatia misingi ya biashara na hawapati vikwazo vya aina yoyote ambavyo vitawafanya washindwe kufanya biashara zao vizuri.

“FCC tunashajihisha na kulinda ushindani, ufanyaji wa biashara nchini unaongozwa na misingi ya biashara uria hivyo kunakua na ushindani kwa watendaji na sisi kazi yetu ni kuhakikisha washiriki wote wanafanya hivyo bila kuumizana Wala kufanya vurugu ambazo zitawafanya wengine wasiweze kufanya shughuli zao vyema”

Erio alisema FCC kazi yao ni kufanya tathmini ya kitaalamu na kuhakikisha kwamba muungano wa makampuni ambazo zinataka kuwekeza nchini hautakua na athari katika kukuza uchumi wa nchi .

“Tunawezesha kampuni ambazo zinataka kuja kufanya biashara au kuwekeza katika nchi yetu kwa misingi ipasayo wanaweza kufanya hivyo hii ni kwasababu kuna njia nyingi ya kuingia kufanya biashara mojawapo ni kuanzisha kampuni na kuungana na kampuni ambazo tayari zipo wale wanaokuja kuungana wanakuja kwetu na sisi kazi yetu ni kufanya tathmini ya kitaalamu na kuhakikisha kwamba muungano wa makampuni hautakua na athari katika kukuza uchumi wa nchi yetu”

“Katika kuangalia kwamba muungano ni mzuri na hauna athari, tunawezesha pia kampuni kuweza kukua na kuendeleza shughuli za kiuchumi kwa utaratibu ambao utakua ni rahisi kwao”

Kadhalika Erio alisema FCC wanamlinda mlaji dhidi ya mbinu hadaifu ambazo zinaweza zikajitokeza sokoni ili mtu apate kitu anachikihitaji na akipate kwa utaratibu ambao ni sahihi na siyo utaratibu wa kulazimishwa kuhakikisha kwamba kilakitu kinakwenda vizuri.

“Katika kumlinda mlaji tunaangalia kwa mfano mkataba ya watu wanaokwenda kukopa katika mabenki waweze kuingia katika mikataba ambayo haiwaathiri au haiwanufaishi wakopeshaji pekee”

“Huwezi kuwa na mkataba mtu anakuja kukopa unaweka kifungu kwenye mkataba kwamba mkopeshaji anahaki ya kubadilisha kiwango Cha riba wakati wowote kuweka masharti ambayo yapo katika lugha ya kigeni pekeyake kiasi kwamba watu hawaelewi, kuweka maandishi madogo ambayo kusomeka hayasomeki hivyo mikataba hiyo tunaipitia tunahakikisha ipo sawa ndiyo tunaruhusu itumike kuhakikisha watu wanaelewa wanapoingia kwenye mikataba na yanayojiri wakati wakiwa kwenye mkataba yanaenda sawa na Yale yaliyopo kwenye mkataba” Alisema Erio