April 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Fahamu umuhimu wa kuwekeza kwa mtoto mwenye umri wa miaka 0-8 kunavyoleta tija

Na Joyce Kasiki,TimesMajira online,Dodoma

MKURIGENZI Idara Idara ya Maendeleo ya Watoto ,Wizara ya Maendeleo ya Jamii,Jinsia na Makundi Maalum Sebastian Kitiku amesema,umri mzuri wa kuwekeza kwa mtoto na kuwa na nguvu kazi bora hasa katika kufikiri,kupambanua mambo na utendaji bora ,ni kuanzia umri wa miaka 0 hadi 8.

Akizungumza kuhusu umuhimu wa kumlea na kumzingatia mtoto katika siku 1000 za mwanzo hadi miaka minane kupitia kipindi kilichorushwa na Radio Dodoma (Dodoma FM) Kitiku amesema,ipo haja kubwa ya kuwekeza kwa mtoto mwenye umri huo kwa lengo la kuhakikisha anakua kwa utimilifu wake.

Kwa mujibu wa Takwimu za idadi ya watu kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) ,jumla watu hapa nchini ni takribani milioni 60 ambapo kati ya hao wenye umri 0-8 ni takribani milioni 16 wakiwemo wavulana milioni milioni 8.3 na wasichana milioni 8.1 ambapo idadi hiyo ni sawa na asilimia 30 ya watu wote.

“Idadi hiyo ni kubwa kwa maana ya idadi ya watu wote waliopo nchini kwa maana ya kuwekeza .”alisema Kitiku

Aidha aliufahamisha umma kuwa ,ukuaji wa ubongo wa binadamu kwa asilimia 90 hufanyika katika kipindi cha kuanzia miaka 0 hadi minane lakini katika kipindi cha siku 1000 ndio unakua kwa haraka zaidi.

“Ubongo wa binadamu unakua kwa asilimia 100,lakini kwa asilimia 90 unakua katrika kipindi cha siku 1000 tu tangu akiwa tumboni,maana yake usipowekeza kumlea mtoto katika kipindi hicho unakuwa umempoteza mtoto kwa maana ya nguvukazi tunayoihitaji kwa kuwa na watu wenye uwezo wa kutafakari mambo kwa haraka,ubunifu na kufikiri.”amesema Kitiku na kuongeza kuwa

“Kwa hiyo uwekezaji wa mtoto katika kipindi cha miaka 0 hadi minane na hizi siku 1000 zikiwemo ,ni muhimu sana kwa watoto wetu katika kufikia utimilifu wao.”

Aidha Kitiku amesema katika malezi ,makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto jamii inatakiwa kuzingatia mambo matano ambayo ni pamoja na Afya bora,Lishe bora,malezi yenye muitikio ,ujifunzaji wa awali na ulinzi na usalama wa mtoto.

“Ili akue vizuri mtoto anahitaji afya bora kuanzia tumboni kwa mama yake,na Serikali imefanya hilo inatoa huduma za afya bure kwa wajawazito na watptp chini ya umri wa miaka mitano.”amesema

Hata hivyo amesema pamoja na jitihada hizo lakini bado kunahitajika msisitizo zaidi wa upatikanaji wa huduma bora za afya kwa mama wajawazito na watoto wadogo..

“Kufuatia utekelezaji wa Programu Jumuishi ya Malezi,Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto sasa tunakwenda kutengeneza Taifa la kujipambanua kufikiri na kutafakari mambo kwa kina na uchapakazi.”

Mdau na mtaalam wa masuala ya malezi,makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto kutoka shirika lisilo la Serikali la CIC –Children in Crossfire linalojishughulisha na malezi na makuzi ya maendeleo ya awali ya mtoto Miriam Kasile amesema,katika mambo hayo matano hakuna lisikuhakikisha mtoto anafikia utimilifu wake.

Kwa upande wake Afisa Lishe kutoka Wizara ya Afya Japhet Mayenga amesema,katika kipindi cha umri wa kuanzia miaka 0 hadi minane,mtoto anatakiwa kupata chakula bora tangu akiwa tumboni kwa mama yake.

“Katika kipindi hicho lishe bora ni muhimu tangu mama akiwa mjamzito kwani inaepusha mtoto kuzaliwa na changamoto mbalimbali za fahamu ikiwemo mgongo wazi na kichwa kikubwa.”amesisitiza

Naye Irene Kweka Afisa Liseh kutoka Wizara ya Afya amesema mtoto baada ya kuzaliwa hadi miezi sita anapaswa kunyonya maziwa ya mama pekee huku akisisitiza mtoto lazima anyone maziwa ya kwanza ya mama mara baada ya kuzaliwa ambayo yana virutubisho muhimu na hutoka siku mbili hadi tatu za mwanzo tu baada ya mtoto kuzaliwa na baada ya hapo hayatengenezwi tena.

Amesema baada ya miezi sita ndipo mtoto aanze kupewa vyakula vya nyongeza kwa kupata milo miwili hadi mitatu inayozingatia makundi matano ya vyakula na aendelee kuongezewa milo kulingana na anavyokua.

Mzazi ambaye pia ni mdau wa masuala ya lishe Barnabas Kisengi amesema,ipo changamoto katika masuala ya lishe katika jamii ambapo huamini baba ndiye anapaswa kula lishe bora kutokana na majukumu yake ya utafutaji wa kipato.

“Pamoja na kwamba jamii imeamka lakini bado kuna changamoto katika jamii zetu,bado kuna akina mama wanaamini kwamba hata akipika kuku,zile nyama nzuri ni za baba huku watoto wakiambulia vipapatio.”amesema Kisengi

Ameiomba Serikali kuendelea kuelimisha jamii kuhusiana na masuala ya lishe hasa kwa watoto wadogo ili waweze kuwa na adya njema lakini pia kuondokana na changamoto mbali za magonjwa yanayoweza kuwakumba kutokana na ukosefu wa lishe.