April 26, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Dkt.Tax:SUMAJKT ipo tayari kushirikiana na wafanyabiashara nchini

Na Penina Malundo,timesmajira, Online

WAZIRI wa Ulinzi, Dkt.Stergomena Tax amesema kuwa Shirika la Uzalishaji Mali la Jeshi la Kujenga Taifa SUMAJKT lipo tayari kushirikiana na wafanyabiashara wengine nchini  kutengeneza bidhaa bora na zenye viwango vinavyohitajika.

Tax amesema hayo leo wakati alipotembelea banda la SUMAJKT lililopo kwenye maonesho ya 46 ya Kimataifa ya biashara yanayofanyika katika Viwanja vya Sabasaba Dar es Salaam, ikiwa nimaadhimisha ya miaka 41 tangu kuanzishwa kwake.

Amesema SUMAJKT ipo tayari kushirikiana na mfanyabiashara mwenye biashara yoyote aliyetayari katika kutengeneza bidhaa zenye ubora na viwango ikiwemo  za vyakula ili ziweze kupenya katika masoko ya nje ya nchi.

“Serikali imefanya jitihada kubwa kama ambavyo Rais Samia Suluhu Hassan amekuwa akitembea maeneo mbalimbali duniani kwa lengo la kututafutia fursa za kibiashara hivyo, ni jukumu letu kuzalisha bidhaa zitakazokubalika kwenye masoko ya nje,” amesema Tax.

Amesema zipo fursa huru za biashara Afrika Mashariki (EAC), Jumuiya ya Maendeleo Kusini kwa Afrika na Umoja wa Afrika ambazo zinahitaji ubora, wingi wa bidhaa na kuzifikisha kwa wakati hivyo watimize matakwa hayo kufanya biashara nchi mbalimbali.

Amesema kubwa SUMAJKT wana viwanda vya kuzalisha bidhaa mbalimbali ikiwemo vya kuzalisha malighafi kwa ajili ya sekta ya kilimo, uchakataji wa bidhaa za ujenzi, samani na huduma mbalimbali za ulinzi bandarini na kuimarisha huduma katika sekta afya, matumizi ya teknolojia katika ulinzi.

“SUMAJKT ni mahali sahihi pa biashara na uwekezaji, zipo shughuli mbalimbali zinazofanyika kwa ajili ya kuchangia uchumi wa nchi yetu. Jukumu la jeshi letu ni kulinda mipaka na uchumi ili kuwa huru jambo ambalo linachagizwa na kujitegemea kiuchumi na kijamii na kubaki imara kama taifa na kutekeleza majukumu mengine,” amesema Tax