April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Dkt. Ndumbaro:Serikali itaendelea kuwaunga mkono watetezi wa haki za binadamu

Na Penina Malundo,timesmajira,Online

WAZIRI wa Katiba na Sheria Dkt.Damas Ndumbaro amesema serikali inaendelea kuhaidi na kuwaunga mkono watetezi wa haki za binadamu nchini kwa kazi wanazofanya ya kusaidia majukumu ya Serikali .

Akizungumza hayo jana jijini Dar es Salaam,Waziri wa Katiba na Sheria Dkt.Damas Ndumbaro akifungua kikao kazi cha kupitisha mpango mkakati wa Asasi za Kiraia kuhusu utekelezaji wa mapendekezo 187 yaliyokubaliwa na Tanzania kwenye duru la tatu la Mchakato wa Tathimini ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa (UPR).

Dkt.Ndumbaro amesema suala la kulinda na kutetea haki za binadamu ni jukumu la Serikali ndo maana hata katika katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Ibara ya 12 hadi 29 ambayo inaongelea suala la haki za binadamu.

” Mtetezi namba moja wa watetezi wa haki za binadamu ni Rais Samia hivyo kazi kubwa inayofanywa na watetezi wa haki za binadamu ni kumsaidia Rais wetu Samia hivyo ni vyema kuhakikisha tunazingatia utanzania kwanza katika kufanya kazi hii,”amesema na kuongeza

“Sisi kama serikali tunawaunga mkono sana Watetezi wa haki za binadamu na tunashirikiana nao kuhakikisha haki za binadamu zinatekelezwa kwa kuzingatiwa Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na Katiba ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwani katiba hizi ni mikataba kati ya wananchi na Serikali zinazowaongoza wananchi na kupitia katiba hizi wananchi wamesema waongozwe vipi,hivyo katika kutetea haki hizi za binadamu inapaswa kutokidhana na Katiba ambayo ni matakwa ya wananchi,”amesema Waziri Ndumbaro.

Amesema Sera,Sheria,Mila, Desturi na Tamaduni za tanzania lazima zizingatiwe katika kutetea na kupigania haki za binadamu.”Serikali inapongeza THRDC kwa kuadhimisha miaka 10 katika utendaji kazi wake,kwani imefanya kazi kubwa na nzuri ya kutetea haki za binadamu kipindi chote cha miaka 10 na tunafurahishwa zaidi na ushirikiano uliopo kati ya mtandao na Serikali katika kipindi chote cha miaka 10,”amesema

Kwa upande wake Ofisa Uchechemuzi Mwandamizi THRDC, Raymond Kanegene amesema wamekutana katika mkutano huo kwa lengo la kupitisha mpango wa utekelezaji wa mchakato wa UPR.

“Mwaka 2021 kwa nchi ya Tanzania mapendekezo yaliyotolewa katika baraza la haki za binadamu ambapo serikali iliyakubali ni mapendekezo 108 lakini Serikali ikatoa fursa tena ya kuangalia mapendekezo mengine ambapo mwaka 2022 na serikali iliongeza mapendekezo mengine na kufikia 187 ,”amesema