May 21, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

DC wa Chemba abwagwa rufaa dhidi ya mkewe

Na Grace Gurisha

MAHAKAMA ya Wilaya ya Ilala, Dar es Salaam, imetupilia mbali rufaa iliyokatwa na Mkuu wa Wilaya ya Chemba, Simon Odunga kupinga hukumu ya Mahakama ya Mwanzo Ukonga iliyoamuru Odunga kutoa sh. milioni saba kama sehemu ya gharama ya matunzo ya kumsomesha mtoto wake.

Aidha, Mahakama imemuamuru Odunga kutoa kiasi cha sh. 100,000 kila mwezi ikiwa ni gharama za matunzo ya mtoto wao.

Uamuzi huo ulitolewa jana na Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya ya Ilala, Glory Nkwera ambaye amekazia hukumu hiyo na kumtaka Odunga kutoa kiasi hicho cha fedha kama ilivyoamuliwa na Mahakama ya Mwanzo ya Ukonga, ambapo fedha hizo ni nusu ya gharama za matunzo aliyotumia mkewe Madelina Mbuwuli kumsomesha mtoto wao kuanzia darasa la kwanza hadi kidato cha sita.

Aidha, Hakimu Nkwera amesema ndoa baina ya wawili hao itabaki kama ilivyo sasa kwa sababu hajaona mahali ambapo mkatiwa rufaa Madelina alikosea, bali mrufani Odunga ndiye alikosea kwa kumtelekeza mwenzake na kuondoka nyumbani, hivyo ndoa ibaki kama ilivyo.

Amesema kuwa Odunga alitakiwa kuonesha sababu za msingi, ambapo angeonesha Madelina alikosea na aliweza kufanya makosa kinyume cha sheria, hivyo mahakama imeona ndoa yao haijavunjika na hakuna sababu za kusema ndoa imevunjika na haiwezi kurekebishika.

Hata hivyo Hakimu Nkwera amesema iwapo kuna mtu hajaridhika na hukumu hiyo ana haki ya kukata rufaa ipo wazi