May 21, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watatu kortini tuhuma za kusafirisha Heroin

Na Grace Gurisha

WATU watatu, Fatuma Mgwani, Omary Khamis na Ahmed Said wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na shtaka la kusafirisha dawa za kulevya aina ya Heroin zenye uzito wa gramu 2099.74 sawa na Kilogramu 2.099.

Hata hivyo, inaelezwa kuwa washtakiwa hao walifanyiwa vipimo vya ugonjwa wa homa kali ya mapafu (COVID-19) unaosababishwa na virusi vya Corona na majibu yameonesha ni wazima hivyo hawataweza kupeleka maambukizi yeyote maabusu.

Washitakiwa hao waliofikishwa mahakamani hapo leo mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi, Rashidi Chaungu na kusomewa mashtaka yao na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Wankyo Simon.

Akisoma hati ya mashtaka, Wakili Simon amedai kuwa, Aprili 17, mwaka huu eneo la Bandari ya Dar es Salaam iliyopo Wilaya ya Ilala, washtakiwa hao walisafirisha dawa za kulevya aina ya heroin zenye uzito wa gramu 2099.74 sawa na Kilogramu 2.099.

Baada ya kusoma mashtaka hayo, Wakili Simon amedai kuwa upelelezi wa shauri hilo bado haujakamilika lakini pia shtaka linalowakabili washtakiwa halina dhamana, hivyo wanaomba tarehe nyingine kwa ajili ya kutajwa kwa kesi hiyo.

Aidha, Simon amedai kuwa, washtakiwa hao walifanyiwa vipimo vya ugonjwa wa homa kali ya mapafu (COVID-19) unaosababishwa na virusi vya Corona na majibu yameonesha kuwa wapo salama, hivyo hawataweza kupeleka maambukizi yeyote maabusu.

Kufuatia kauli hiyo Hakimu Isaya ameahirisha kesi hiyo hadi, Mei 13, mwaka huu na kuwaamuru washitakiwa kwenda maabusu kwa kuwa kesi yao haina dhamana.