May 1, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Cioaba awashauri TFF kuongeza wachezaji wa akiba

Na Mwandishi Wetu

KOCHA Mkuu wa klabu ya Azam FC, Aristica Cioaba, ameliomba Shirikisho la Soka Nchini (TFF) kuongeza idadi ya wachezaji wa akiba kutoka watatu wa awali hadi watano.

Cioaba ametoa ombi hilo kwa TFF akiwa na malengo ya kuwasaidia wachezaji wake pamoja na timu nyingine kujiepusha na majeraha, endapo Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) itarejeshwa.

Hadi sasa tayari umeshapita zaidi ya mwezi mmoja toka Serikali ilipotangaza kusimamisha shughuli zote za michezo kutokana na jamba la virusi vya ugonjwa wa Corona ambao idadi wa wagonjwa inaongezeka kila kukicha.

Awali Serikali ilitangaza kusimamisha shughuli hizo za michezo kwa siku 30 ambapo mechi za mwisho zilizechezwa machi 17 siku ambayo serikali ilitangaza kusimamisha michezo lakini kutokana na kuongezeka kwa idadi ya wagonjwa hao, imetangaza kuendelea kusimamisha shughuli hizo kwa muda usiojulikana.

Lakini kabla ya Serikali kusimamisha michezo hiyo, tayari Ligi ilikuwa imesimama kupisha maandalizi ya timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ iliyokuwa kambini kujiandaa na mashindano ya Kombe la Mataifa Afrika kwa Wachezaji wa Ligi ya Ndani (CHAN) iliyopangwa kuanza Aprili 4 hadi 25 ambayo pia Shirikisho la soka Afrika (CAF) waliihairisha baada ya ongezeko la wagonjwa wa Corona (COVID-19) barani Afrika.

“Tunaiomba TFF kuangalia kama kuna uwezekano wa kutuongezea idadi ya wachezaji wa akiba katika mechi kutoka wale watatu wa awali hadi watano ili kuwasaidia kuwaepusha na majeraha wanayoweza kuyapata kwani ni muda sasa wanafanya mazoezi ya kawaida na si yale ya ushashindani yanayowapa stamina ya kuhimili ushindani wa mechi,” alisema kocha huyo.

Hata hivyo baadhi ya wadau wa soka hapa nchini wameonesha wasiwasi wao na kudai kuwa huenda viwango vya wachezaji hao vikashukwa kwani licha ya kupewa programu binafsi za mazoezi lakini ni ngumu kuendelea kulinda viwango vyao kwa aina hiyo ya mazoezi.

Wadau hao walisema kuwa, kwa aina ya wachezaji wa hapa nchini ili timu kucheza kwa ushindani basi ni lazima wachezaji wafanye mazoezi kwa pamoja ambayo yatawapa muunganiko mzuri lakini hili la kila mmoja kufanya mazoezi yake binafsi kunaweza kushangia baadhi yao kushindwa kuonesha kile walichokuwa nacho awali.

Hali hilo pia ilifanya baadhi ya makocha wa Ligi mbalimbali iliwemo Ligi Kuu kuiomba TFF endapo Ligi itaruhusiwa kuendelea basi wangeomba muda wa zaidi ya wiki mbili za maandalizi ili kujipanga upya na kutengeneza muunganiko mzuri wa vikosi vyao jambo pia litakalowaepusha wachezaji wao na majeraha yasiyo la lazima.