May 8, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

CCM yamlilia Jaji Mark Bomani

Na Penina Malundo, TimesMajira Online, Chato

CHAMA cha Mapinduzi CCM, kimetoa salamu za pole na rambirambi kufuatia kifo cha aliyewahi kuwa Mwanasheria Mkuu wa Kwanza wa Tanzania , Jaji Mstaafu Mark Bomani aliyefariki katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Akitoa salamu hizo Wilayani Chato koani Geita, Katibu wa Nec Itikadi na Uenezi wa Chama hicho,Humphrey Polepole amesema Chama chao kimepokea kwa masikitiko makubwa msiba wa Jaji Bomani ambaye amedumu ndani ya Chama hicho muda mrefu na aliyewahi kuwa Mwanasheria Mkuu wa kwanza nchini.

Akimuelezea Jaji Bomani ,Polepole amesema amekuwa kada wa chama cha mapinduzi kwa muda mrefu na kuwahi kuomba kuteuliwa kuwania nafasi ya urais ndani ya Chama kipindi cha nyuma lakini hakupata uteuzi.

“Jaji Bomani alikuwa mwanachama mwaminifu na mtiifu ndani ya CCM pia amedumu kama mjumbe wa Baraza la wadhamini ndani ya Chama hivyo kwetu huu ni msiba mkubwa kwa kuondokewa na Kada mtiifu Jaji Bomani pia napeleka pole kwa umma wa watanzania kwa msiba huu,” amesema Polepole.

Hata hivyo, Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema kuwa kifo cha Jaji Mstaafu Mark Bomani ni pigo kubwa kwa sekta ya sheria na kwamba watahakikisha wanamuenzi kwa kutekeleza yale yote aliyoyaishi na kuyaanzisha.

“Jaji Bomani mara zote alikuwa anasisistiza kwamba sheria zinatungwa ili zitekelezwe, hivyo ni jambo ambalo tutalazimika kama sehemu ya kumuenzi ni kuyaishi kutekeleza zile sheria mabzo alizianzisha na kuzifanyia kazi hadi kufikia hatua ya kutumika,”amesema Dkt.Chemba.

Jaji Bomani alizaliwa Oktoba 22 mwaka 1943, huko Wete visiwani Pemba jijini Zanzibar.