May 14, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

CCM yamlilia Bantu, Muhina

Na Mwandishi wetu, TimesMajira, Dodoma

CHAMA Cha Mapinduzi CCM , kimepokea kwa masikitiko na huzuni kubwa taarifa ya kifo cha Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) kutoka Mkoa wa Morogoro, Hassan Mamba (Bantu) kilichotokea Hospitali ya Taifa Muhimbili pamoja na kifo cha Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Mkoa wa Tabora Mwajuma Muhina kilichokea katika Hospitali ya Wilaya Nzega Mei 18,2021.

Taarifa iliyotolewa na Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa Idara ya Itikadi na Uenezi,Shaka Hamdu Shaka kwa vyombo vya habari ,ilisema Mwenyekiti wa Chama hicho ambaye ni Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amevitaja kwa pamoja vifo hivyo kuwa ni msiba mzito kwa Chama chao.

Amesema wamepoteza viongozi hao wawili ambapo Chama kiliwategemea, kuwatumaini na kunufaika nao kwani walikuwa wanasiasa hodari, wazoefu na wachapakazi.

“Kazi ya Mwenyezimungu haina makosa, kupoteza kwao maisha wakati huu ni jambo la kusikitisha kwani ni wakati ambao ushauri wao, upeo na maarifa waliyokuwa nayo katika kufanikisha kazi na mipango ya kisiasa, kioganaizesheni na kisera ilikuwa ni msaada mkubwa kwa Chama Cha Mapinduzi,”amesema

Amesema Chama Chao kinatoa pole kwa familia, ndugu, jamaa, marafiki na wanachana wa CCM Mkoa wa Morogoro na Tabora kwa kuwapoteza Viongozi wao wapendwa.