May 17, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

CCM kushika dola Dar es Salaam 2024 /2025

Na Heri Shaaban , TimesMajira Online

MBUNGE wa Viti Maalum Mkoa Dar es Salaam Janeth Masaburi, amesema chama cha Mapinduzi CCM kitashika dola kwa kushinda majimbo yote mkoa Dar es Salaam uchaguzi wa Serikali za mitaa na uchaguzi mkuu wa Rais wabunge na madiwani.

Mbunge Janeth Masaburi alisema hayo wilayani Ubungo katika ziara yake ya utekelezaji wa Ilani ya chama cha Mapinduzi CCM na kuangalia Miradi ya maendeleo na kutoa elimu ya kutumia nishati ya gesi alipokuwa akiwagawiwa majiko ya gesi mama lishe.

“Chama cha Mapinduzi CCM kimejipanga vizuri katika uchaguzi wa Serikali za mitaa mwaka 2024 na Uchaguzi mkuu mwaka 2025 nawaomba wana CCM mjenge Umoja na mshikamano ndio ushindi wa chama chetu CCM katika uchaguzi zote alisema Masaburi.

Mbunge Masaburi aliwataka viongozi wa chama na Jumuiya wa wilaya ya Ubungo kufanya kazi kwa weledi wajiepushe na Rushwa wasimame imara.

Aidha pia aliwataka wafanye ziara katika miradi ya Serikali kuangalia utekelezaji wa Ilani ya chama cha Mapinduzi CCM kwa kazi kubwa inayofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan.

Katika hatua nyingine aliwataka wananchi waliojenga mabondeni kuondoka maeneo hatarishi wasijenge nyumba mabondeni wala kuweka makazi mvua hizi za EL NINO ni kubwa zinaendelea kunyesha kama tulivyotangaziwa na wataalam wetu wa hali ya hewa TMA.

Pia aliwataka wananchi wa Wilaya ya Ubungo kujenga tabia ya utunzaji mazingira kwa kupanda miti ya matunda na miti ya vivuli sambamba na kujenga tabia ya kuwa wasafi katika mazingira yao waepuke uchafu.