May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

BREAKING NEWS:Mbunge Lusinde mikononi mwa TAKUKURU

Na Doreen Aloyce,TimesMajira Online,Dodoma

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Dodoma imekiri kumhoji Mbunge anayemaliza muda wake wa Jimbo la Mtera mkoani Dodoma, Livingstone Lusinde (Kibajaji) baada ya kupata taarifa za Mbunge huyo kuwakusanya wajumbe wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Chamwino na kuwahonga.


Hatua hiyo imekuja kufuatia usiku wa kuamkia jana kuzuka taarifa za kushikiliwa kwa Mbunge huyo sambamba na baadhi ya wajumbe na wanachama wa CCM.

Akizungumza na TimesMajira Online, Kamanda wa Takukuru Mkoa wa Dodoma, Sosthenes Kibwengo amekiri kumhoji kwa saa mbili Mbunge huyo na kumuachia na kwamba uchunguzi zaidi juu ya tuhuma hizo bado unaendelea.


Kibwengo amesema ofisi yao ilipata taarifa za Mbunge huyo kuwakusanya wajumbe wa mkutano mkuu wa Chama wa wilaya na wale wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Wilaya ya Chamwino kwa lengo la kuwapatia fedha kwa ajili ya ushawishi ili wamsaidie kwenye kampeni zake za ubunge.


”Hakuwekwa ndani ila tulimhoji katika ofisi zetu za Takukuru Wilaya ya Chamwino kwa masaa mawili au matatu hivi, na taarifa tulizopata ni kwamba anakusanya watu na kuwahonga hatukupata ushahidi wa yeye kuhonga, lakini uchunguzi wa hilo jambo bado unaendelea,”amesema Kibwengo.


Hata hivyo Kibwengo amesema uchunguzi dhidi ya tuhuma hizo unaendelea na kadri TimesMajira Online itakavyokuwa ikipata mrejesho.