April 28, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Bil. 44.9 kutumika halmashauri ya Karatu 2024/25

Na Sophia Fundi, Timesmajira Online, Karatu

HALMASHAURI ya wilaya ya Karatu mkoani Arusha, imepanga kutumia kiasi cha Sh. bilioni 44.9, katika mwaka wa fedha wa 2024/25, bajeti ambayo imepokelewa kwa shangwe na madiwani pamoja na wananchi wa wilaya hiyo.

Kiasi hicho cha fedha kimepitishwa jana na madiwani katika kikao maalum kilichofanyika kwenye ukumbi wa hospital ya wilaya, Karatu.

Akisoma rasimu ya bajeti hiyo, mchumi mwandamizi kwa niaba ya Mkurugenzi, Rosemary Samson amesema bajeti hiyo imepanda kwa asilimia 9, ukilinganisha na bajeti ya mwaka 2023/24, ambayo ilikuwa Sh. bilioni 43.8 kutokana na udhibiti wa makusanyo ya mapati, ushuru wa mabango pamoja na maengesho ya magari.

Akisoma mchanganuo wa bajeti hiyo, Rosemary amesema kati ya kiasi hicho mishahara ni Sh. bilioni 26.3, sawa na asilimia 58, matumizi mengineyo Sh. bilioni 1.1 sawa na aslimia tatu, vyanzo visivyolindwa Sh. bilion 5.1 huku vyanzo lindwa Sh. bilioni 1.2 sawa na aslimia 15 na miradi ya maendeleo Sh. bilioni 10.9 swa na asilimia 24.

Rosemary amesema, halmashauri kutoka mapato yake ya ndani imepanga kukusanya na kitumia Sh. bilioni 6.6 kwa mwaka wa fedha 2024/25, kiasi ambacho kinalenga kukamilisha miradi mbalimbali ya maendeleo katika wilaya hiyo.

Naye mwenyekiti wa halmashauri hiyo, John Lucian amewapongeza wataalam kwa mchakato mzima wa bajeti pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo na madiwani kwa kupitisha bajeti hiyo ya kishindo.

Amesema, bajeti hiyo imelenga zaidi kutekeleza miradi mbalimbali katika kila kata kwa kukamilisha miradi viporo ambayo ni maelekezo kutoka kwa viongozi wa juu, Mkuu wa wilaya na Mkuu wa Mkoa ili kuepusha hoja za ukaguzi.

Hata hivyo, amewataka madiwani kusimamia utekelezaji wa bajeti hiyo ambayo itakuwa ya mwisho wao kuwa madarakani, hivyo kuwasihi kila diwani kusimamia vyema eneo lake.

“Madiwani wenzangu mjue hii bajeti ni ya mwisho kwetu, kila diwani ahakikishe anasimamia vyema miradi itakayoenda kutekelezwa hasa miradi ya viporo kwani kila kata imetengewa bajeti yangu,” amesema Lucian.

Baadhi wa ya wananchi waliojiwa na kusema, wamefurahishwa sana bajeti hiyo ambayo itakuwa ya kuhistoria kwani imegusa kila kata kutekeleza miradi viporo.

Pia, wamepunguza ushuru mbalimbali ikiwemo ushuru wa mazao kuwa Sh. 2000 kiasi kinachofanana pamoja na ushuru wa mazao ya biashara kuwa Sh. 3000 bila kutenganisha aina ya mazao.ya biashara kuwa Sh. 3000 bila kutenganisha aina ya zao.

“Tunawapongeza madiwani kwa kupitisha rasimu hii kwanza, bajeti ni ya kishindo kwani wamepunguza ushuru wa mazao kuanzia mwaka wa fedha 2024/25, sasa ushuru ni mmoja tu wa mazao ya biashara na mazao ya chakula,” amesema Paulo Akonaay ambaye ni mkulima.