May 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Benki ya Maendeleo ya wanawake Rukwa kuwakomboa wanawake

Na Israel Mwaisaka, TimesMajira Online, Rukwa

WANAWAKE mkoani Rukwa wamedai kuwa uanzishwaji wa benki ya Wanawake mkoani Rukwa kutachagiza maendeleo ya haraka na jamii kuweza kujikwamua kiuchumi.

Wakizungumza kwenye mkutano wa mchakato wa uanzishwaji wa benki hiyo Wanawake (Rukwa Women Agrofactory Bank) wa kata za Kirando na Itete wilayani Nkasi walisema kuwa wao wapo tayari juu ya uanzishwaji wa benki hiyo na kuwa itawaondoa kwenye utumwa wa mikopo ya rib

Mmoja wa Wanawake hao Sophia Bazir alisema kuwa wameelewa vyema malengo ya uanzishwaji wa benki hiyo ya Wanawake mkoani Rukwa na kuwa wao sasa wapo tayari kuwa wanachama na wanahisi kama mchakato wake unachelewa na kuomba ukamilike haraka ili waweze kuitumia benki hiyo kujikwamua kiuchumi.

Alisema kuwa wao kama Wanawake wajasiliamali wamekuwa wakijiingiza kwenye mikopo ya riba kubwa kutoka kwenye taasisi mbalimbali za kifedha na mwishowe ujikuta wakizinufaisha taasisi hizo na wao kujikuta wakiendelea kuwa masikini.

Q

Asia Stephano kwa upande wake alidai kuwa wameridhishwa na maelezo na malengo ya benki hiyo kubwa alilolibaini ni kutaka kumuomboa Mwanamke na kuuomba uongozi wa benki hiyo uharakishe mchakato wa uanzishwaji wake ili ianze kazi na wao waitumie katika shughuli zao za kiuchumi.

Mwenyekiti wa mchakato wa uanzishwaji wa benki hiyo Emmy Paul Sikazwe alisema kuwa mchakato wa uanzishwaji wa benki hiyo umekamilika na upo katika hatua ya mwisho kikubwa ni kuwataka Wanawake kuunga mkono jitihada hizo ili benki hiyo ianze kufanya kazi.

Alisema kuwa benki ya Wanawake lengo lake kuu ni la ukombozi kwa Wanawake hiyo imetokana na vilio vingi vya Wanawake kunyang’anywa thamani za ndani na hata kuuziwa nyumba zao pindi wanapochelewa kurejesha mikopo yenye riba kubwa kwenye taasisi mbalimbali za ukopeshaji na kujikuta wakiingia kwenye migogoro katika ndoa zao.

Mratibu wa mchakato huo Hillaly Musa kwa upande wake aliwataka Wanawake kuwa wamoja katika kuijenga benki yao na kuwa wasiyumbishwe na watu wasiotaka maendeleo yao na kuwa benki ya wanawake ni mkombozi kwao.

Dues Chege ambaye ni baba wa familia alisema malengo ya benki hiyo ni mazuri kwani yamekuja kuzikomboa familia ila aliitaka benki hiyo kuwapatia kwanza elimu ya ujasiliamali Wanawake kabla ya kupewa mikopo ikiwa ni pamoja na kuwaambia umuhimu wa ndoa kwani wengi wao wakiwa na uchumi ndoa nyingi uvurugika.