May 1, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

BAWACHA: Wanaopinga Katiba mpya Tume, hawakupingi, wanakupima

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online, Moshi

KATIBU wa BAWACHA Taifa, Carherine Ruge, amesema wanaompiga Rais Samia Suluhu Hassan katika dhamira yake ya kuhakikisha inapatikana Katiba Mpya na Tume Huru ya Uchaguzi ndani ya CCM, hawampingi bali wanampima.

Ruge ametoa kauli hiyo wakati akitoa salamu BAWACHA kwenye kongamano la Siku ya Wanawake Duniani, ambapo Rais Samia alikuwa mgeni rasmi.

Amesema wanawake hao wameweza kujenga baraza la wanawake lenye nguvu, wapambanaji, wenye ushawishi, hivyo uwepo wake kwenye kongamano hilo ni sehemu sahihi.

Alisema kwa mujibu wa Sensa aliotangaza mwenyewe wanawake ni jeshi kubwa, wapo milioni 31. Amesema wanawake ndio walipa kodi wakubwa, lakini hadhi yao na watoto havifanani.

Alisema pamoja na mazuri yanayoyafanywa na Rais Samia, kupitia kongamano hilo atafungua sikio na kusikia yale ambayo wanawake wenzao wa CCM hawamuambii.

“Yale ambayo yanahitaji utashi wako ambayo haujayasikia, utayasikia,” amesema Ruge. Amesema pamoja na jitihada zake za kujenga Tanzania ya haki, lakini wapo wanaojaribu kukwamisha na wengi wao ni wanaume na BAWACHA wanamwambia usiache.

Amesema mwanamke akidhamiria jambo lake atafanikisha kwa juhudi zote. Alisema wanatambua jitihada zake za kutaka kupata katiba mpya na tume huru ya uchaguzi kabla ya uchaguzi wa mwaka 2025.