April 30, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Askofu Mwamalanga aridhishwa na miaka mitatu ya Rais Dkt. Samia

Na Mwandishi Wetu,TimesmajiraOnline,Dar

MWENYEKITI wa Kamati ya Kitaifa ya Maaskofu na Mashehe ya Maadili Amani na Haki za Binadamu kwa Jamii ya Madhehebu ya Dini nchini, Askofu William Mwamalanga, amesema kwa kipindi cha miaka mitatu, Rais Samia Suluhu Hassan, ameonesha uwezo mkubwa kwenye uongozi pamoja na kuwakomboa wanawake kisiasa.

Askofu Mwamalanga, alitoa kauli hiyo jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki wakati akizungumzia uwezo wa Rais Samia kwenye uongozi katika kipindi cha miaka mitatu.

Rais Samia alishika wadhifa huo Machi, 2021 kufuatia kifo cha Rais John Magufuli.

Alisema kwa miaka mitatu ameimarisha uhuru wa wanasiasa, vyombo vya habari na Watanzania kwa jumla, huku akiwajengea wanawake uwezo wa kujiamini na kuwabadilisha kimtazamo.

“Tunaona hata uwezo wa walinzi wake wanawake, huko nyumaa hakuna aliyekuwa akijua uwezo wao hii imefanya wanawake kujiamini pale wanapopewa nafasi,” alisema Askofu.

Askofu Mwamalanga amewahimiza wanawake kwenye vyama vya siasa kutembelea vijijini na kufanya mikutano na akina mama badala kujikita kwenye kumbi za viyoyozi.

Alisema Rais Samia ameonesha uwezo mkubwa wa kufikia maLengo ya ukombozi kwa wanawake, kwani mwanamke anahitaji kujikomboa kifikra kisiasa na kiuchumi.

“Kwa sasa amefaulu sana kuwakomboa wanawake kisiasa hapa anatakiwa kushikwa mkono na wanawake wenye uwezo kifedha na matajiri kwa kumsaidia mwanamke wa kijijini,” alisema Askofu Mwamalanga.

Naye Alhaji Waziri Mwenda kutoka Tabora na Mlei Eva Kihwele. walikiri kwamba kwa miaka mitatu ya uongozi wa Rais Samia, amejitahihidi kuwaunganisha wanawake kwenye ajira za siasa na makundi ya wafanyabiashara.

“Mwanamke ingawa anatakiwa kushuka chini vijijini ambako mwanamke anahitaji mkombozi mkubwa wa maisha vijijini hakuna anayegusa maisha ya mwanamke huko ni wakati wa kubadili kama taifa,” alisema.