April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Asasi zatakiwa kuhamasisha ushiriki zoezi la Sensa 2022

Na Zena Mohamed, Timesmajiraonline, Dodoma.

KAMISAA wa sensa ya watu na makazi Spika mstaafu Anne Makinda amezitaka Asasi za kiraia nchini(AZAKI),kushirikiana na Serikali kuhamasisha Wananchi kushiriki kikamilifu Katika zoezi la Sensa ya watu na makazi litakalofanyika kufanyika ifikapo  Agosti 2022. 

Makinda amesema hayo leo wakati akitoa mada ya uelimishaji na uhamasishaji  wa masuala ya sensa kwa Asasi za Kiraia Katika Mkutano wa wiki ya AZAKI unaoendelea Jijini hapa.

Ameeleza kuwa umuhimu wa sensa unagusa Kila nyanja hivyo ni wajibu kwa kila mtanzania kuisadia Serikali kupata taarifa za msingi zitakazosaidia mchakato wa utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya mwaka 2025, mageuzi ya masuala ya afya na jamii, pamoja na ufuatiliaji wa ajenda za maendeleo za kimataifa.

“Sensa ya Watu na Makazi ni zoezi la kitaifa linalofanyika kila baada ya miaka 10 ambapo Sensa ya mwisho kufanyika nchini ni ile ya mwaka 2012 hivyo Sensa ya mwaka huu  itakuwa ni sensa ya sita kufanyika nchini baada ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar mwaka 1964. Sensa nyingine zilifanyika mwaka 1967, 1978, 1988, 2002 na 2012,Sensa ni muhimu na nyinyi watu wa AZAKI ni wadau namba moja ,tunatakiwa kutoka kwenye uchumi wa Kati tuendende zàidi tufanane na wenzetu,”ameeleza.

Amesema sensa ya watu na makazi ni utaratibu wa kukusanya, kuchambua, kutathimini na kuchapisha na kusambaza takwimu za kidemographia, kiuchumi na kijamii kuhusiana na watu wote na makazi yao katika nchi kwa kipindi maalum,kwa maana nyingine, sensa ni zoezi maalum lenye lengo la kupata idadi ya watu wote katika nchi.

Pia kwa umri na jinsia, mahali wanapoishi na hali yao ya elimu, hali ya ajira, hali ya vizazi na vifo na hali ya makazi. Takwimu hizi za msingi ndiyo zinazoweza kuanisha mahitaji halisi ya wananchi yakiwemo makundi maalum yenye uhitaji maalum kwa mfano, watu wenye ulemavu, wanawake, watoto, vijana na wazee hivyo kurahisisha uandaaji wa sera na mipango ya maendeleo kulingana na uhitaji na mazingira.

Kutokana na hayo Kamisaa huyo wa sensa ameeleza upekee wa Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022 kúwa utazingatia taarifa za idadi ya watu husaidia katika mamlaka za wilaya katika utekelezaji wa mipango ya maendeleo ambayo huakisi matakwa ya watu katika ngazi husika na kusaidia kwenye uwiano wa mgawanyo wa rasilimalimali.

“Taarifa za sensa zitawezesha serikali kujua ongezeko la idadi ya watu, kwa mgawanyo na viashiria vingine, ambavyo ni muhimu kwa usimamizi wa mazingira,msingi wa utawala bora na ujumuishaji wa demokrasia,takwimu hizi zinahitajika kwa ajili ya ugawaji wa majimbo ya uchaguzi kwa ufanisi, kurekebisha mipaka ya kiutawala katika serikali za mitaa,”amefafanua.

Naye Mtakwimu Mwandamizi,Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) David Mwaipopo

amesema sensa ya mwaka 2022 kama zilivyo sensa zilizopita itatumia aina mbili kuu za madodoso ambazo ni dodoso refu litakalotumika kuhoji asilimia 30 ya maeneo yote ya kuhesabia watu na Dodoso fupi litakalotumika kuhoji kwenye asilimia 70 ya maeneo yote ya kuhesabia watu.

Ameyataja madodoso mengine kuwa ni  la Taasisi ambalo ni mahsusi kwa ajili ya wasafiri, waliolala mahotelini/nyumba za wageni, na waliolazwa hospitalini na dodoso la Wasio na Makazi maalum ambalo ni mahsusi kwa watu wote wanaolala maeneo yasiyo rasmi, kwenye baraza za majengo mbalimbali, kwenye madaraja na maeneo mengine.

“Utekelezaji wa sensa ya watu na makazi hufanyika katika awamu kuu tatu kuu ambazo ni kipindi kabla ya kuhesabu watu, wakati wa kuhesabu watu na kipindi baada ya kuhesabu watu,”amesisitiza.

Licha ya hayo Mtakwimu huyo Mwandamizi amefafanua maswali yatakayoulizwa wakati wa sensa ya Watu na Makazi mwaka huu huku akieleza kiwa moduli kumi na nne zitatumika kukusanya taarifa za watu na makazi yao nchi nzima.

 “Maswali hayo ni tarifa za kidemografia (umri, jinsi, uhusiano, hali ya ndoa, uraia, Maswali yanayohusu ulemavu;tarifa za Elimu;maswali ya uhamaji, pamoja na taarifa za Watanzania wanaoishi nje ya nchi,mengine ni maswali kuhusu umiliki wa nyaraka za kitaifa (vitambulisho vya NIDA, Mzanzibari mkazi, cheti cha kuzaliwa, hati ya kusafiria, na leseni ya udereva),shughuli za kiuchumi na umiliki wa ardhi na taarifa za TEHAMA,”amesema.

Pia ametaja maswali mengine yatakayoulizwa kipindi cha sensa  kuwa ni tarifa za uzazi na vifo vilivyotokea ndani ya kaya,vifo vitokanavyo na uzazia,hali ya nyumba za kuishi na umiliki wa rasilimali mbalimbali,maswali ya kilimo na mifugo pamoja na mifuko ya hifadhi ya jamii.

“Tunaomba AZAKI mshiriki kikamilifu kuelimisha jamii tufikie malengo,sisi kama Ofisi ya Takwimu tumejipanga vizuri kwa kutumia rasilimali chache zilizopo ili kukamilisha kwa wakati shughuli zote za maandalizi ikiwamo kazi ya utengaji wa maeneo ya kuhesabia watu katika ngazi ya kitongoji na mtaa ambayo ndiyo msingi wa kufanikisha sensa kwa ubora,”ameeleza.