April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Aliyekimbia kifungo anaswa, kufungwa miaka 30 Jela

Na Stephen Noel, Mpwapwa

MKAZI wa Mpwapwa, Julias Lwagila, aliyekuwa akisakwa na Polisi baada ya kukimbia kifungo cha miaka 30 hatimaye ametiwa mbaroni ikiwa ni utekelezaji wa amri ya Mahakama ya Wilaya Mpwapwa.

Lwagila alihukumiwa kifungo cha miaka 30 akiwa hayupo mahakamani na Hakimu Mkazi  Wilaya ya Mpwapwa Mkoa wa Dodoma baada ya kumtia hatiani kwa kujihusisha na kilimo cha bangi na kuhifadhi madawa hayo.

Hukumu hiyo iliyotolewa mwaka jana, lakini baada ya mshtakiwa huyo kuona mwenendo wa kesi ulivyokuwa unaelekea siku ya hukumu hakutokea mahakamani, hivyo kuhukumiwa bila kuwepo mahakamani.

Baada ya hukumu hiyo mahakama iliamuru Polisi kumtafuta popote alipo mshtakiwa huyo ili aendelee na adhabu yake.

Hukumu hiyo iliyotolewa na aliyekuwa Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya Mpwapwa, Paschael Mayumba ambaye alihamishiwa Mahakama ya Wilaya ya Dodoma.

Hakimu Mayumba ameelezea kuridhishwa na ushahidi dhidi ya mshtakiwa huyo  kuhusiana na kukamatwa kwake na Polisi wilayani Mpwapwa wakati wa msako wa kusaka dawa za kulevya.