May 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

ACT yajitosa sakata la Plea Bargaining

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online

CHAMA cha ACT Wazalendo kimeshauri kwamba wakati wakati Watanzania wakisubiri ripoti ya ukaguzi wa fedha na utaratibu wa kesi zilizohitimishwa kwa kufuata sheria ya makubaliano ya kukiri kosa (Plea Bargaining) ni muhimu hatua za uwajibishaji zichukuliwe ili kulinda heshima ya Ofisi ya Umma.

Ushauri huo ulitolewa jana na Msemaji wa Sekta ya Katiba na Sheria ya ACT Wazalendo, Victor Kweka, kupitia taarifa yake kwa vyombo vya habari.

Kweka alisema ACT Wazalendo wanapendekeza hatua zifuatazo kuchukuliwa;

Moja, Rais Samia Suluhu Hassan aunde Tume ya majaji, ili kupitia malalamiko ya watu wote ambao walilipishwa fedha kwa mtindo wa kukiri makosa na kulipa fedha Serikalini.

Pili, chama hicho kimeshauri wale watakaobainika walilazimishwa   kukiri makosa warejeshewe fedha zote.

Aidha, chama hicho kimemtaka Jaji Biswalo Mganga ajiuzulu ili kupisha uchunguzi wa tuhuma dhidi yake.

Nne, chama hicho kimeshauri Jaji Kiongozi asimpangie kazi Jaji Biswalo Mganga hadi uchunguzi utakapokamilika na kujua hatma ya maamuzi ya uchunguzi wa fedha za Plea Bargain. 

Ushauri wa chama hicho unafuatia kuibuka tena kwa taarifa za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Charles

Kichere, zinazohusu kuendelea na uchunguzi wa akaunti ya fedha   zilizokusanywa kutokana na utaratibu wa makubaliano ya kukiri kosa ‘plea bargaining’.

Kwa mujibu wa chama hicho ripoti yake inatarajiwa kutolewa Machi 2023. Hatua hiyo imechochea mjadala na kuzalisha mapendekezo tofauti tofauti kutoka kwa kikiwemo chama hicho.