Na Mwandishi Wetu, Timesmajiraoneli, Dar
AIRTEL Tanzania imezindua rasmi huduma ya Airtel Chapakazi, suluhusho jipya lililoundwa kuchochea ukuaji wa wajasiriamali na wafanyabiashara wadogo kote nchini.
Uzinduzi wa huduma hiyo uliofanyika jana, Julai 16, mwaka huu Makao makuu ya Airtel Tanzania jijini Dar es Salaam, ulionesha dhamira ya Airtel katika kukuza maendeleo jumuishi ya kidijitali na kuunga mkono ajenda ya kukuza uchumi wa Tanzania.
Airtel Chapakazi inalenga kuinua biashara ndogo ndogo kwa kuwawezesha wajasiriamali kote nchini kutumia teknolojia kama daraja la kufikia masoko mapya, wateja wapya na fursa zaidi za kukuza kipato.
Kulingana na takwimu za kitaifa, asilimia 15 tu ya biashara ndogo ndogo na za kati nchini Tanzania kwa sasa zinapata zana rasmi za masoko ya kidijitali, pengo ambalo Airtel Chapakazi inalenga kuziba. Airtel Chapakazi ni suluhisho la kibunifu linaloenda kuwapa wafanyabiashara wadogo uwezo sawa wa kidijitali unaotumiwa na makampuni makubwa.
Huduma ya Airtel Chapakazi inapatikana katika vifurushi vitano vilivyoundwa kulingana na ukubwa na mahitaji na utofauti wa biashara:
SME chap pack ( sh.100,000): Inajumuisha laini 2 za simu, kila moja ikiwa na GB10 ya data, SMS 1,000, na dakika 1,000 kwa mitandao yote. Pia kifurushi hiki kinajumuisha router ya intaneti ya bure kwa ajili ya matumizi ya ofisi yenye kasi ya 10 Mbps
Kifurushi cha SME Bomba (sh. 150,000): Inajumuisha laini 3 za simu, kila moja ikiwa na 10GB ya data, SMS 1,000, na dakika 1,000 kwa mitandao yote. Pia kifurushi hiki kinajumuisha router ya intaneti ya bure kwa ajili ya matumizi ya ofisi yenye kasi ya 20 Mbps.
Fahari Pack (sh. 200,000): Inajumuisha laini 5 za simu, kila moja ikiwa na 10GB ya data, SMS 1,000, na dakika 1,000 kwa mitandao yote. Pia kifurushi hiki kinajumuisha router ya intaneti ya bure kwa ajili ya matumizi ya ofisi yenye kasi ya Mbps 30 na SMS 5,000.

Supa Pack (sh. 300,000): Inatoa laini 9 za simu zenye data sawa, SMS, na manufaa ya sauti, router ya ofisi ya bure ya Mbps 30, na SMS 10,000 kwa wingi.
Max Pack (sh. 400,000): Inatoa laini 14 za simu, router ya ofisi ya bure yenye kasi ya Mbps 50, na SMS 15,000 — zinazofaa kwa timu kubwa yenye watu wengi au yenye ukuaji wa kasi ya juu.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkurugenzi wa Biashara wa Airtel Tanzania, Joseph Muhere, alisema Airtel Chapakazi inadhihirisha dhamira ya Airtel kusaidia biashara ndogo ndogo na za kati kupitia huduma suluhishi za kidijitali.

“Kwa kutumia Airtel Chapakazi, wateja watapata msaada wa karibu kutoka kwa mawakala wetu kuanzia hatua ya mwanzo hadi kupakua programu kutoka Play Store. Baada ya taarifa hizo kuthibitishwa, mteja atapokea ujumbe mfupi wa kiunganishi wa kupakua programu ya Airtel Chapakazi kutoka Play Store, mteja atapakua programu hiyo, kuchagua kifurushi: Fahari, Supa, au Max, na kukamilisha malipo ili kuwezesha huduma.” Alieleza Muhere.
Muhere alisisitiza juu ya umuhimu wa biashara ndogo ndogo na za kati katika uchumi wa Tanzania, akibainisha kuwa kundi hilo la wafanyabiashara wajasiriamali linashikilia zaidi ya asilimia 95 ya biashara zote, limeajiri zaidi ya watu milioni 8, na linachangia takriban asilimia 35 kwenye Pato la Taifa, ilhali wengi bado hawajafikiwa na zana za kijiditali ambazo zinaweza kukuza biashara zao kwa kiasi kikubwa.
“Kwa kipindi kirefu, Airtel Tanzania ilikuwa na dhamira ya kuanzisha suluhisho la kidijitali ambalo litaboresha sekta ya biashara na kuchangia katika kukuza uchumi wa nchi na sasa ndoto hiyo imetimia kwa kupitia Airtel Chapakazi,” aliongeza Muhere.
Uzinduzi wa Airtel Chapakazi ni sehemu ya dhamira kubwa ya Airtel Tanzania katika kukuza maendeleo jumuishi, yanayoendeshwa na teknolojia nchini kote kwa kuwapa wafanyabiashara wanazohitaji ili kustawi katika zama za kidijitali.

More Stories
Kihenzile ahamasisha uwekezaji sekta ya anga
Wafanyabiashara watuliza wananchi hofu ya bei ya bidhaa
TISEZA kuanzisha madawati ya uwekezaji kila Halmashauri za Wilaya