October 2, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TIC: Ushupavu wa Samia wazidi kuleta wawekezaji

Na Jackline Martin, TimesMajira Online

KITUO cha Uwekezaji Tanzania (TIC) kimesema uongozi mahiri na shupavu wa Rais Samia Suluhu Hassan, umefanikisha kituo hicho kusajili miradi 198 ya uwekezaji kati ya Aprili- Juni  2024 yenye thamani ya Dola za  Marekani Bilioni 1.6 ya zaidi ya sh. Trilioni 3 .

Hayo yamesemwa jana na Mkurugenzi Mtendaji TIC, Gilead Teri, wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, alipokuwa akiwasilisha ripoti yao ya siku za hivi karibuni kuhusu mwenendo  wa hali ya uwekezaji nchini Tanzania

“Mafanikio na maendeleo hayo makubwa yanayotokana na sehemu kubwa ya uongozi mahiri na shupavu wa Rais Dkt. Samia  kutokana na kutambua kwake kwamba uwekezaji ni moja ya nyenzo kubwa sana ambayo inaweza kuleta ukuaji wa uchumi ,lakini pia kuondoa umasikini miongoni mwa Watanzania,” alisema Teri. 

Miradi hiyo ya uwekezaji inatarajiwa kuzalisha ajira mpya takribani 96,000 nchini

|Hilo ni ongezeko la asilimia 53.49 ya idadi ya miradi iliyosajiliwa ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka 2023 ambapo miradi 129 pekee yenye thamani ya Dola za Marekani bilioni 1.007 ilisajiliwa na hivyo kuzalisha ajira 14,631,” alisema.

Aidha, alisema kati ya Aprili- Juni 2023 kituo cha uwekezaji Tanzania kilisajili miradi 129 yenye thamani ya uwekezaji wa takribani dola Bilioni 1 inayotarajia kuleta ajira 14,000 nchini

 “Kwenye hili tunaona ongezeko la mitaji pekee zaidi ya asilimia 60, ongezeko la miradi pekee takribani asilimia 53 na matatajio ya ajira takribani asilimia 500,” alisema.

 Pia Kati ya Aprili – Juni 2023 kituo hicho kilisajiri miradi 129,pia miradi 198 kwa mwaka 2024 yenye mitaji ya dola bilioni 1.6

Aidha, alisema Mwaka 2023 kati ya Julai – Septemba miradi 137 ilisajiliwa ambapo kwa  sasa kuna ongezeko la takribani asilimia 100 kufikia miradi 256 na mitaji ya dola bilioni 3.9.

Akizidi kufafanua siri ya mafanikio hayo, Teri alisema; ” Hayo ni matokeo mazingira bora ya uwekezaji kwenye sheria, kanuni na taratibu.

Lakini pia utendaji kazi wa Taasisi za Serikali ambazo zinasimamia kuwezesha mazingira ya uwekezaji nchini,” alisema

Kadhalika, Teri alisema mafanikio hayo ni kazi kubwa  inayofanywa na balozi za Tanzania kote duniani ambao wanakutana na wawekezaji kila siku na kufanya juhudi za kuwavutia na kuwashawishi kuhusu kuwekeza Tanzania.

“Tunampongeza Rais Samia kwa kuipambania Tanzania kupitia diplomasia ya uchumi  ya kimataifa, uwezo wake wa uongozi, sera zake na sheria ambazo amezitunga katika nchi yetu ambazo zinafanya Tanzania kuwa kimbilio kwa wawekezaji wa nje pamoja na wa ndani kwa kuleta neema hii ya mitaji pamoja na ajira kwa Watanzania wote,” alisema.

“Tunawapongeza mabalozi ambao ni wawakilishi nje ya nchi waliokuwa mstari wa mbele kushawishi na kuvutia. Uwekezaji nchini,” alisema.