September 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Rais,akerwa tuhuma zinazolikabili jeshi la Polisi

Na Martha Fatael,Moshi, Timesmajira Online,Moshi

RAIS Dkt.Samia Suluhu Hassan ameonesha kukerwa na tuhuma, zinazolikabili Jeshi la Polisi nchini, kuhusu vitendo mbalimbali vinavyotishia tunu ya amani na utulivu nchini.

Kufuatia hali hiyo Dkt Samia amesema kamwe hatamuonea aibu,mtu yeyote anayeratibu, anayeshiriki na kutekeleza mipango miovu inayohatarisha kutoweka kwa amani na utulivu.

Rais Dkt Samia amesema hayo, Septemba 17,2024 wakati akifunga kikao kazi cha Maofisa Waandamizi wa Jeshi la Polisi,kilichoenda sambamba na maadhimisho ya miaka 60 ya kuanzishwa kwa Jeshi hilo, yaliyofanyika shule ya Polisi Moshi(MPA).

“Jeshi la Polisi,kama mlinzi wa raia na mali zake, halipaswi kuhisiwa ama kushukiwa katika ukiukwaji wa sheria na haki inayozisimamia!,jisahihisheni hapo,” amesema Dkt.Samia na kuongeza:

“Mfano ‘clip ya video’ iliyotokea jijini Mwanza,inaonesha raia wamezuia polisi wasimchukue mhalifu hadi Mkuu wa kituo cha polisi (OCS) afike.Hatua hiyo ni mbaya,mnapaswa kujisafisha ili kujenga imani kwa wananchi kuhusu usalama wao na si vinginevyo,”.

Sanjari na hayo,Rais Samia,amelitaka Jeshi la Polisi, kuongeza imani kwa wananchi juu ya sheria na haki wanazosimamia,Pia watumie teknolojia ya habari na mawasiliano kukabiliana na uhalifu wa aina yoyote.

Katika hatua.nyingine Dkt Samia ameitaka Wizara ya Mambo ya Ndani na Jeshi la Polisi,kutekeleze mapendekezo ya Tume ya Haki Jinai,kuhusu namna bora ya kuimarisha taasisi za kijinai.

Huku akitaka, utekelezaji wa mapendekezo yote yasiyohitaji mabadiliko ya sheria au ongezeko la bajeti pamoja na Jeshi la Polisi,kusimamia maadili ya askari wake,ili kuwatoa katika tuhuma zinazolichafua jeshi hilo.

Katika maadhimisho ya miaka 60 ya Jeshi la Polisi,tuzo na nishani zilitolewa kwa maofisa 10, waliotumikia Jeshi hilo kwa zaidi ya miaka 40.Kati yao walishiriki vita ya Kagera mwaka 1978 na wengi walistaafu.