Na Sophia Fundi, Timesmajira Online,Karatu
Halmashauri ya Wilaya ya Karatu mkoani Arusha imepanga kufunga kamera za ulinzi (CCTV Camera)katika maeneo mbalimbali ya makusanyo ya mapato ndani ya Wilaya hiyo. Lengo likiwa ni kuwadhibiti watumishi wasiowaaminifu.
Hayo yamebainishwa na Madiwani wa Halmashauri hiyo, hivi karibuni katika kikao cha Baraza la Madiwani kilichofanyika katika ukumbi wa Halmashauri hiyo.

Akizungumza Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Karatu, John Lucian, amesema kuwa kumekuwa na watumishi wasiowaaminifu katika maeneo ya makusanyo ya mapato ya Halmashauri.Hivyo ni jukumu la Halmashauri kuthibiti mapato yake.
Madiwani hao kwa pamoja wameridhia kamera hizo, kufungwa maeneo ya geti za ukusanyaji wa ushuru,hospitali ya Wilaya,vituo vya afya na baadhi ya zahanati zenye watu wengi.Lengo ni kuthibiti fedha za serikali na kuwabaini watumishi ambao siyo waaminifu katika kazi zao.
Wamemwagiza Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo,kuhakikisha zoezi la kununua kamera hizo linakamilika ndani ya mwezi huu na zifungwe katika maeneo yote yanayoingizia mapato Halmashauri.
“Mkurugenzi tunakupongeza, kwa k kutembelea maeneo ya geti zetu za ushuru bila kujali muda,umekuwa ukitembelea maeneo hayo hata usiku bila kujali,tunakupongeza sana kwa kazi nzuri unayofanya”Amesema Lucian.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Juma Hokororo, amewahakikishia Madiwani kutekeleza maazimio yote ya vikao, likiwemo la kununua kamera ,huku akiwaomba ushirikianao kwenye kata zao katika kutekeleza miradi mbalimbali.

More Stories
Utafiti wafichua mazito sekta ya uvuvi baharini
Takwimu Rasmi kuongoza utekelezaji Dira 2050
TBS kuadhimisha miaka 50,kuzindua kitabu chake