September 23, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TRA ilivyojipanga kuwahudumia wananchi maonesho 88

Na Joyce Kasiki,Times majira online,Dodoma

AFISA Mwandamizi Kodi wa Mamlaka ya Mapato nchini (TRA) Philipo Eliamini amewaasa wananchi wote wanaotembelea maonesho ya wakulima na wafugaji (88) kufika katika banda lao ili waweze kupata elimu kuhusiana na masuala ya kodi pamoja shughuli mbalimbali zinazofanywa na Mamlaka hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari Agosti 2, 2024  katika viwanja vya 88 Nzuguni jijini Dodoma,Waliamini amesema maonesho hayo yanatoa fursa kwao kuonana na wananchi kuwapa elimu ikiwemo ya masuala ya kukodi,masuala ya usimamizi wa kodi lakini pia inapokea maoni na malalamiko ya wananchi ambayo pia kuwawezesha kuboresha utendaji wao wa kila siku.

“Kwa hiyo tunasema maonesho haya ni fursa nzuri kwa wananchi kujifunza lakini pia ni fursa nzuri kwetu ambapo tunaweza kuonana na wadau wetu na tunawapa elimu ambayo itawasaidia katika shughuli zao.”amesema Eliamini  

Ameongeza kiwa “kama mnavyofahamu wadau wa maonesho haya ni ya wakulima na tunasema kilimo ni biashara,lakini tunafahamu serikali imewekeza kwa kiasi kikubwa sana kwenye masuala ya kilimo lakini pia inatoa misamaha mbalimbali kwenye eneo la kilimo matarajio ni kwamba wakulima hawa wanapofanya shuguli hizo na kupata kipato kitakachofikia kiwango cha kutozwa kodi basi na wao waweze kuichangia serikali katika masuala mazima ya kodi”

Amesema  kila mwaka serikali kupitia Bunge inafanya mabadiliko ya sheria mbalimbali ikiwemo sheria za kodi na kwamba , kwa mwaka huu wa fedha 2024/2025 kumefanyika mabadiliko mbalimbali ya kikodi ambapo,kwa upande  wa sheria za kodi kuna misamaha mbalimbali ya kodi ambayo inaenda kuleta unafuu mkubwa kwa wakulima. 

Vilevile amesema wanayatumia maonesho hayo kutoa namba ya utambulisho wa mlipa kodi kufuatia mabadiliko ya sheria ya mwaka jana ambayo yaliweka kipengele cha kila raia kuanzia umri wa miaka 18 na kuendelea anapaswa kuwa na namba hiyo  ya utambulisho wa mlipa kodi ambapo muhusika anapaswa kuwa na namba ya kitambulisho cha Taifa (NIDA).

Eliamini alisema,pia wanatoa huduma ya makadirio ya kodi kwa mfanyabiashara ambaye bado hajakadiriwa makadirio ya kodi kwa mwaka huu wa fedha lakini pia kwa wanaodaiwa kodi na wanahitaji kupata namba za malipo huduma hiyo inapatikana. 

“Wasambazaji wa mashine za kutolea risiti za EFD na zile za VFD,wanatoa elimu ya matumizi ya mashine hizo na wataalam wapo, na mashine zipo kwa wanaohitaji kununua ,ambapo kila mfanyabiashara mwenye mauzo ya kuanzia ahilingi milioni 11 kwa mwaka anapaswa kununua na kutumia mashine hizo.”amesema Eliamini