September 21, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Hifadhi ya Burigi kuimarisha Ulinzi wa wanyamapori kwa kutumia” Drone “

Na Penina Malundo, Timesmajira

KAMISHNA wa Uhifadhi wa Shirika la hifadhi za Taifa (TANAPA) Juma Kuji amesema hifadhi ya Burigi Chato imeanza kutumia teknolojia za kisasa kulinda hifadhi kwa kutumia ndege zisizo na rubani(Drone).

Hatua hiyo imekuja baada ya mifugo mbalimbali kutoka nchi Jirani kuingia katika mbuga hiyo na kuzuia majangili wanakuja kuwinda wanyamapori katika hifadhi hiyo.

Amesema wejipanga kuongeza doria katika hifadhi ili kuhakikisha wahalifu wanakamatwa na kufikishwa katika vyombo vya Sheria na kuzuia kabisa hali ya uvamizi na ujangili katika eneo hilo.

“Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) imejipanga kukomesha matukio ya ujangili na uvamizi wa Mifugo hifadhini ndio maana tumeanza kutumia teknolojia za kisasa kulinda hifadhi kwa kutumia ndege zisizo na rubani na nyingine ili kuhakikisha wahalifu wanakamatwa,”amesema.

Kamishna kuji ametoa wito kwa wananchi kuacha mara moja tabia za kuingia hifadhini na kufanya uhalifu ikiwemo kuingiza Mifugo katika maeneo hayo kwani lazima watakamatwa .

Naye Mkuu wa wa hifadhi hiyo, Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi,Ismail Omar amesema Ulinzi wa hifadhi hiyo sasa umeimarika hali ambayo inasabisha utulivu wa Wanyamapori na Wanyamapori kuanza kuongezeka.

Omar amesema ,changamoto ambayo wanaendelea Kuidhibiti ni kuingizwa mifugo kutoka nchi jirani na baadhi ya viongozi wa vijiji wasio waadilifu .

“Tuna vijiji 38 vinavyozunguka hifadhi sasa baadhi ya maeneo kuna viongozi wanapokea wafugaji kutoka nchi jirani na kuingiza Mifugo hifadhini hasa katika maeneo ya milima na mabonde”amesema

Hata hivyo, amesema kutokana na matumizi ya Teknolojia za kisasa katika Ulinzi Mifugo imekuwa ikikamatwa na kufikishwa Mahakamani.

“Tunaomba viongozi wachache wa vijiji waache kuhujumu hifadhi na wajuwe lazima tutawakamata wao na Mifugo iliyoingizwa hifadhini”amesema.

Naye ,Afisa Uhifadhi Mkuu wa ldara ya Ulinzi,Deogratius Mwageni amesema kukamatwa kwa Mifugo hiyo ni kutokana na kuimarika Ulinzi na akaonya baadhi ya viongozi wa vijiji kushirikiana na wahalifu kuingiza Mifugo hifadhini.

Mwanasheria na Kitengo cha uchunguzi na kuendeshaji kesi katika hifadhi ya Burigi -Chato, Emmanuel Zumba amesema wamekuwa na operesheni ya kukamata Mifugo hifadhini kuanzia Julai 2024 hadi sasa,wamekamata Ng’ombe zaidi ya 1000 na wanakesi 165 na hadi sasa 74 zimetolewa uamuzi ambapo wameshinda.