October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Niyonzima ‘fiti’ kuwavaa Kagera, Morrison ndani

Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online, Kagera

BAADA ya juzi mashabiki wa Yanga kupata hofu kuwa huenda wasimuone katika mechi kadhaa kiongo wao fundi, Haruna Niyonzima, Daktari wa timu hiyo, Shecky Mngazija ameshisha presha hiyo na kudai yupo fiti hata kutumika katika mchezo wao wa kesho dhidi ya Kagera.

Niyonzima aliumia dakika ya nne baada ya kuchezewa rafu na mchezaji wa Biashara na mwamuzi aliwaita Daktari ambao walimpatia huduma ya kwanza na kisha kumtoa nje.

Baada ya kupatiwa huduma hiyo, Niyonzima alirudi uwanjani kuendelea na mchezo lakini alishindwa kuendelea na mechi baada ya kudondoka chini nakutolewa nje akiwa kwenye machela na nafasi yake kuchukua kiungo, Mzanzibar Abdulaziz Makame ‘Bui’.

Kabla ya taarifa hiyo ya Dkt. Mngazija, kocha mkuu wa Yanga, Luc Eymael, amesema kuwa, Niyonzima atakosa mechi mbili muhimu dhidi ya Kagera Sugar na ile ya Julai 12 dhidi ya Simba.

Lakini jana Dkt. Mngazija aliweka wazi kuwa, huduma walizompatia Niyonzima zilikuwa nzuri na hadi jana asubuhi alikuwa sawa hivyo mashabiki na wanachama hawapaswi kuwa wa wasiwasi na hali yake.

Amesema, kiungo huyo pamoja na wachezaji wengine waliopata maumivu kwenye mchezo huo dhidi ya Biashara wanaendelea vizuri ambao ni pamoja na nahodha Msaidizi Juma Abdul na Abdulaziz Makame

“Tunaendelea kumpatia matibabu na hadi leo (jana) asubuhi yuko sawa, hivyo mashabiki na wanachama wasiwe na wasiwasi juu ya hali yake, kwani kama ataendelea vyema zaidi anaweza kutumika hata katika mchezo unaofuata dhidi ya Kagera Sugar,” amesema Dkt. Mngazija.

Kuelekea kwenye mchezo huo tayari jana jioni kikosi cha Yanga kimewasili mkoani Kagera tayari kwa ajili ya mchezo wao wa kesho ambao umerudishwa nyuma kwa siku moja kwani awali ulitakiwa kuchezwa Julai 9.

Baada ya kuwasili Kagera, makocha walisimamia mazoezi mepesi ya wachezaji hasa kwa wachezaji ambao hawakupata majeruhi na ambao hawakutumika jana.

Viongozi wa benchi hilo la ufundi wamesema kuwa, baada ya mazoezi hayo mepesi, leo kikosi kitaanza kufanya mazoezi ya kiufundi kwenye uwanja wa Kaitaba ili kujiweka sawa kuwakabili wenyeji wao.

Hata hivyo Yanga wanajipa nafasi kubwa ya kuondoka na alama tatu baada ya Winga wao Bernard Morrison kujiunga na wenzake jana kwa ajili ya kuongeza nguvu kuelekea kwenye mchezo huo.

Morrison ambaye hakusafiri na wenzake waliowakabili Biashara United aliondoka Dar es Salaam jana asubuhi na jioni alifaanya mazoezi mepesi na wenzake.

Awali kocha Eymael hakuweka wazi sababu za kutosafiri na Morrison licha ya kuwepo kwenye mipango yake na kudai kuwa iwapo atamuhitaji kwenye mchezo dhidi ya Kagera Sugar atawaambia viongozi wampeleke.

Kupitia ukurasa wake wa Istagram Morrison ameandika kuwa, “habari Bukoba, niambieni kile ambacho sijaskia ‘Hellooo Bukoka Now tell me what I’ve not heard before’.