October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

CHABAMI waiangukia Serikali, wadau wa michezo Iringa

Na Zuhura Zukheir, Timesmajira Online, Iringa

WANACHAMA wa chama cha waendesha baiskeli Mkoa wa Iringa (CHABAMI) wameiangukia Serikali na wadau wa michezo mkoani kuwasaidia kiuchumi ili waweze kuendeleza mcheo huo.

Mmoja wa wanachama wa CHABAMI, Hassan Malufu ameuambia Mtandao wa Timemajira kuwa, moja ya malengo yao makubwa ni kuona siku za mbeleni wanafanikiwa kushiriki mashindano ya mbio za baiskeli ya kutaifa na kimataifa

Amesema, wao kama wanamichezo wanatamani pia kuona mchezo huo unatambulika zaidi kwa jamii kama ilivyo kwa michezo kama soka ambao unafahamika hadi kwa watoto wadogo, kikapu na riadha.

Malufu amesema, kwa sasa viongozi wa chama hicho wanatakiwa kutafuta wafadhili watakaowashika mkono pindi yanapotokea mashindano ndani na nje ya Mkoa wa Iringa ikiwa pamoja na ushiriki wa mchezo huo wa mbio za baiskeli nje ya nchi.

“Jambo kubwa ambalo tunalihitaji kwa sasa ni kuona viongozi wetu wanazidisha jitihada za kutafuta wadhamini ambao wataweza kusaidia chama kuandaa mashindano mbalimbali ya ndani ya Mkoa ambayo yatatuimarisha ili hata ikitokea kunakuwa na mashindano ya kitaifa na kimataifa tuweze kuwakilisha vena Mkoa na nchi kwa ujumla,” amesema Malufu.

Mmoja wa viongozi wa chama hicho, Yupiana Mbogela amesema, kwa sasa chama chao bado ni kichanga na kina idadi ndogo ya wanachama hivyo kama kuna mtu atakuwa tayari kujiunga basi watampokeo kwa mikono miwili ili kuungana kusukuma mbele gurudumu la waendesha baiskeli Mkoani hapo.

Amesema, licha ya kuwa wamejiunga na mchezo wa kuendesha lakini wamekuwa wakijishughulisha na kazi zingine zinazowaingizia kipato cha kila siku.