October 2, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

EWURA yaridhishwa mradi wa maji kupitia fedha za CSR

Na Judith Ferdinand,TimesMajira Online

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji ( EWURA) imeridhishwa na utekelezaji wa fedha zilizotumiwa na Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Kahama (KUWASSA) kwa ajili ya kurejesha huduma kwa jamii (CSR).

Ambapo KUWASSA wametekeleza mradi wa kuunganisha maji kwa baadhi ya shule zilizopo wilayani humo huku takribani wanafunzi 1,500 wananufaika na mpango huo.Hayo yamebainishwa na Meneja wa EWURA Kanda ya Ziwa George Mhina alipokuwa akikagua utekelezaji wa miradi katika shule ya Sekondari ya Kabela Gold iliyopo Kata ya Mwine wilayani Kahama mkoani Shinyanga.

Mhina ameeleza Kuwa Machi Mwaka 2022 EWURA ilitoa fedha kiasi cha milioni 15 kwa KUWASSA kama tuzo baada ya kuibuka mshindi wa pili kati ya Mamlaka 26 za Mkoa zilizopitwa na kushindanishwa katika utoaji wa huduma za maji safi na usafi wa mazingira Tanzania Bara. kwa Mwaka wa fedha 2020/021.

Ameeleza kuwa shule nyingine zilizonufaika na fedha hizo ni shule za Sekondari Bugisha na Mama Kalembo pamoja na shule ya watoto yenye uhitaji maaalum ambapo zaidi Zaidi ya wanafunzi 1,500 wamenufaika na mpango huo.

Kwa upande wake Mhandisi Maginge Marwa kutoka KUWASSA alieleza kuwa shule zilizonufaika na mradi huo ni zile ambazo ziko takribani kilometa moja na zaidi toka bomba kuu la KUWASSA lilipo hivyo ingewachukua muda mrefu kuzifikia kwa kutegemea bajeti ya KUWASSA.

Wakieleza kwa nyakati tofauti Walimu Wakuu wa shule za Bugisha na Kaleba Sekondari wameishukuru EWURA kwa kupeleka huduma ya maji katika shule hizo Kwani imesaidia kupunguza utoro wa wanafunzi na kuboresha mazingira ya shule kwa kupanda miti na usafi wa vyoo na madarasa.

Huku wanafunzi wakieleza kuwa upatikanaji wa uhakika wa maji safi na salama shuleni umewasaidia kuepukana na magonjwa kama UTI na ya tumbo.

Mmoja wa wanafunzi wa shule zilizonufaika na mradi wa kuunganishiwa maji shule uliotekelezwa na KUWASSA kupitia fedha za CSR, akizungumza na waandishi wa habari.
Baadhi ya wanafunzi wa shule zilizonufaika na mradi wa kuunganishiwa maji shule uliotekelezwa na KUWASSA kupitia fedha za CSR,wakimsikiliza Meneja wa EWURA Kanda ya Ziwa George Mhina hayupo pichani wakati alipotembelea shuleni hapo kwa ajili ya kujionea namna mradi huo uluvyotekelezwa.