Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online
MAMLAKA ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA), kwa kushirikiana na Wakala wa Huduma za Misitu (TFS) pamoja na kamati ya ulinzi na usalama mkoa wa Tabora, imefanya operesheni maalum katika hifadhi ya msitu wa Igombe river iliyopo wilaya ya Uyui.
Lakini pia, katika hifadhi ya msitu wa Nyahua iliyopo wilaya ya Skonge mkoani Tabora na kufanikiwa kuteketeza ekari 68 za mashamba ya bangi, kukamata gunia 133 za bangi huku watu saba (7) wakikamatwa katika operesheni hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari leo tarehe 30 Aprili, 2026 katika ofisi za mkuu wa mkoa wa Tabora, Kamishna Jenerali Aretas Lyimo amesema, Mamlaka iko kwenye operesheni maalum ya kuteketeza dawa za kulevya zinazozalishwa nchini.
“Sasa hivi tuko kwenye kampeni maalum kuhakikisha kwamba tunateketeza dawa za kulevya zinazozalishwa nchini baada ya dawa za viwandani kupungua,” amesema Lyimo.
Aidha, amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuiwezesha Mamlaka kuanzisha ofisi za DCEA kanda ya Magharibi yenye makao yake mkoani Tabora, hatua ambayo imeongeza ufanisi na kasi katika kudhibiti dawa za kulevya nchini.

Sambamba na hilo, Kamishna Jenerali Lyimo ameushukuru uongozi wa mkoa kwa kuunga mkono na kushiriki operesheni hiyo iliyofanikisha ukamataji na uteketezaji wa bangi zinazolimwa katikati ya mapori na hifadhi za taifa mkoani humo.
“Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya hatutakubali uhalifu huu uendelee.
“Tutahakikisha tunafanya operesheni endelevu katika maeneo yote na kuchukua hatua za makusudi kwa watu wanaolima na kuzalisha dawa za kulevya ndani na nje ya mapori,” amesisitiza Lyimo.

Kwa upande wake mkuu wa mkoa wa Tabora Dkt. Paul Chacha, ameipongeza Mamlaka kwa kazi nzuri ya udhibiti wa dawa za kulevya inayoendelea mkoani humo.
Dkt. Chacha amewaagiza askari wa TFS kuweka kambi katika mapori na maeneo ya hifadhi ili kumaliza kabisa tatizo la bangi katika mkoa wa Tabora.

More Stories
Mapinduzi saratani Mbeya kwa takwimu sahihi
Wajumbe wa Bodi ya REA waipongeza ETDCO
Bodi ya REA yaridhishwa na kasi ya usambazaji umeme Mbeya