April 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Zao la Kahawa lakua kwa kasi nchini

Penina Malundo, TimesMajira Online

WAZIRI wa Kilimo Profesa Adolf Mkenda amesema kuwa, zao la Kahawa nchini limekua kwa kiasi kikubwa na kufanya Watanzania wengi kupenda kunywa kinywaji hicho.

Pia amewaondoa hofu wakulima wa zao hilo kuhakikisha wanalima zao hilo kwani asilimia kubwa ya watanzania wameanza kupenda kunywa kahawa kwa wingi na kufanya zao hilo kuzidi kutambulika zaidi.

Waziri Mkenda amesema hayo wakati wa uzinduzi wa siku maalum ya Kahawa nchini kwenye maonesho ya 45 ya Biashara ya Kimataifa Dar es Salaam (DITF) maarufu kama Sabasaba yanayoendelea kwenye Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam ambapo amesema kuwa wataendelea kushikamana na Bodi ya Kahawa kama ilivyo kwa bodi nyingine kwani kuna sehemu wakulima wameshaanza kukata tamaa wanaona zao hilo halilipi.

“Nampongeza ndugu yangu Amir Hamza Kahawa ya Amimza utaikuta madukani Nairobi inauzwa, tungependa kuona Kahawa yetu ina sheheni kwenye masoko makubwa ya Afrika Kusini, Angola, Namibia, Botswana, Zimbabwe, Tunisia tuende hadi China, amesema.

Kwa Upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Kahawa Tanzania,Prof. Aurelia Kamuzora amesema kuwa kampeni ya unywaji wa kahawa unafuata mnyororo wa thamani mkulima anavutwa na wanywaji kama hawatakuwepo kilimo cha kahawa kitakwama.

“Kunywa kahawa kuna faida zake ambapo zao hili lina zaidi ya faida 100 ambazo mnywaji wa kahawa akinywa anazipata katika mwili wake,”amesema Mwenyekiti huyo.

Prof.Kamuzora amesema unywaji wa kahawa angalau kikombe kimoja kwa siku inasaidia ubongo kufanya kazi na kadri unywaji wa kahawa unavyoongezeka ndivyo mkulima anafaidika.

“Namshukuru waziri wa viwanda na biashara Prof. Mkumbo kwa kufanya mazingira mazuri ya uwekezaji watu wanajitokeza kuchukua leseni za kuanzisha biashara za kahawa,” ameongeza kuwa, “tafadhali tafuteni leseni ili mfanye biashara tuvute kilimo kwani huwezi kutenganisha biashaa ya kahawa na kilimo ” ameongeza Prof. Kamuzora.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa bodi hiyo Priscus Kimaryo amesema miaka ya nyuma kahawa ilikuwa inazalishwa kwenye nchi zinazoendelea na kutumiwa katika nchi hizo lakini kwa sasa hadi nchi zinazolima nazo zinatumia kahawa.

“Kwa mfano nchi ya Brazili ni ya kwanza kwenye uzalishaji na ni ya pili kwa unywaji wa kahawa duniani ukiachia Marekani, nchi zinazozalishwa zenyewe zina kunywa kahawa kwa Tanzanai utamaduni wa kunywa ulikuwa zaidi kwenye mikoa ya Pwani na visiwani Zanzibar,kwa hivi sasa asilimia kubwa ya unywaji upo kwenye vijiwe na kwamba Tanzania ina viwanda 28 vya kukaanga imetoka kwenye kuacha kukoboa na kwenda kwenye viwanda vya kukaanga kagawa,”amesema