September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Zahera afunguka kilichowaponza Gwambina

Na Angela Mazula, TimesMajira Online

MKURUGENZI wa Ufundi wa timu ya Gwambina inayoshiriki Ligi Kuu Tanzania Bara (VPL), Mwingi Zahera amesema licha ya kikosi chao kucheza vizuri katika mchezo wao wa juzi dhidi ya Simba lakini bado walionesha hali ya kutojiamini jambo ambalo si zuri kwao.

Zahera ametoa kauli hiyo baada ya kumalizika kwa mchezo kati ya timu yake na Simba uliochezwa kwenye uwanja wa Mkapa ambao walipoteza kwa goli 3-0.

Zahera amesema kuwa, walikuwa wakiwa wamejiandaa kushinda mchezo huo lakini kutokana na hali ya wapinzani wao kwa mara ya kwanza waliona kuwa wanakwenda kupoteza mchezo kutokana na wapinzani wao kucheza vizuri na kutengeneza nagasi nyingi.

Amesema, kutojiamini kwa wachezaji wao ndio kulikowakwamisha dhidi ya Simba hivyo watakachokwenda kukifanya ni kuendelea kuwajenga ili kuwa bora zaidi katika mechi zao zijazo kwani malengo yao yalikuwa ni kucheza mechi 10 ili kujua nini wafanye.

Zahera amesema kuwa, pia mchezo huo umedhihirisha kuwa hawaogopi timu yoyote hivyo timu watakazokutana nazo kuanzia sasa zijipange kwani moja ya maeneo wanayokwenda kuyafanyia kazi ni eneo la ushambuliaji.

“Tutahakikisha tunalishughulikia jambo hili katika mazoezi hivyo jambo hili linaweza lisionekane tena katika mechi zetu zijazo za Ligi Kuu, ” amesema Zahera.