May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wizara ya Afya yataja mikoa inayoongoza kwa tatizo la usikivu nchini

Na Esther Macha, TimesmajiraOnline,Mbeya

WIZARA ya afya imeitaja mikoa mitano inayoongoza Kwa tatizo la usikivu nchini huku mkoa wa Kilimanjaro ukiwa kinara.

Hayo yamesemwa leo,Machi 4,2025 na waziri wa afya Ummy Mwalimu ambaye amewakilishwa na Mwakilishi wa wizara ya Afya Dkt.Maisara Karume wakati wa maadhimisho ya siku ya usikivu duniani ambayo kitaifa imefanyika mkoani Mbeya katika viwanja vya hospitali ya rufaa kanda ya Mbeya.

Dkt.Karume amesema kuwa katika tatizo hilo la usikivu mkoa wa Kilimanjaro unaongoza kwa asilimia 7.4 ikifuatiwa na mkoa wa Ruvuma (5.5),Njombe 5.4),Songwe( 5.2) pamoja na mkoa wa Lindi wenye asilimia (5.0).

“Lakini pia tatizo hili la usikivu inaonyesha kuwa wanawake wana tatizo zaidi la usikivu kutokana na maumbele yao ikilinganishwa na wanaume “amesema Dkt.Karume.

Hata hivyo Dkt Karume ameeleza kuwa tafiti zilizofanyika hapa nchini zinaonyesha kuwa kwa kila watoto wachanga 200 wanaozaliwa mmoja sawa na asilimia 0.5 wana tatizo la usikivu na kwamba kwa upande wa wanafunzi wa shule za msingi utafiti unaonyesha kuwa asilimia 3.17 tatizo la usikivu.

Aidha Mwakilishi wa waziri wa afya Dkt.Karume amesema serikali kupitia mpango wa elimu mashuleni kwa kushirikiana na wadau itaendelea kufanya upimaji wa usikivu ili watakaotambuliwa mapema wahudumiwe ili kuzuia ukiziwi.

Akielezea zaidi Dkt.Karume amesema kupoteza kusikia husababisha na sababu mbalimbali ambazo ni magonjwa, mtoto kuzaliwa na matatizo ya usikivu ,mawimbi makubwa ya sauti ikiwemo mashine zinazotoa mlio mkubwa,matumizi mabaya ya vifaa vya kusikilizia Muziki.

Dkt.Godlove Mbwanji ni Mkurugenzi mtendaji wa Hospitali Rufaa ya Kanda ya Mbeya amesema kuwa changamoto ya usikivu ni tofauti ni ulemavu mwingine hauonekani kwa macho hivyo ni vema kutumia maadhmisho hayo kutoa mapendekezo na maoni , wataalamu kuendelea na mikakati ya kutoa elimu ili kuzuia changamoto hiyo mfano kwenye saluni za kiume kupigwa mziki kuwa kiwango cha juu ambapo wateja hawajui hatma yao.

“Nafikiri wataalamu wetu Wana kazi ya kuendelea kutuelimisha lakini kama ikibidi upande wa sheria na kanuni ziwepo kutusaidia sababu ni vizuri kutibu lakini ni vizuri zaidi kuzuia”amesema Dkt Mbwanji.

Kwa upande wake Dkt.Benedict Ngunyale ambaye ni Daktari bingwa wa masikio,pia hospitali ya rufaa kanda ya Mbeya amesema kuwa upande wa masikio,pia, na koo wataalamu wameongezeka kutoka madaktari bingwa 7 kwa mwaka 2002 hadi 93 mpaka sasa na kwamba wataalamu wa kupima usikivu kutoka wawili mpaka 24 na kusema kuwa kutokuwa na mtaalam wa lugha na tiba matamshi hata mmoja mwaka. 2002 Hadi 10 mpaka sasa.

Aidha Dkt.Ngunyale ametoa mapendekezo kwa hospitali zote za mikoa ziwe na madaktari bingwa wa masikio,pua, na koo, mtaalam wa kupima usikivu na kufundisha lugha na tiba matamshi pamoja na vifaa tiba vya msingi na mashine za kupima usikivu.

Mmoja wa wananchi waliofika katika maadhimisho hayo ,Angelina Juma amesema baadhi ya watu wamekuwa na matatizo ya usikivu hususani watoto wadogo wazazi kuishia kwenye dawa za miti shamba kudhani wamerogwa na hivyo kufanya tatizo hilo la usikivu kuendelea kuwa kubwa na kupelekea kupata matatizo makubwa kutokana na kutopata tiba kwa wakati.