September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waziri Ummy kuzindua Ripoti ya Viashiria vya utafiti wa afya ya uzazi na mtoto na viashiria vya Malaria wa mwaka 2022 Dodoma,kesho

Na Zena Mohamed,Timesmajiraonline,Dodoma.

WAZIRI wa Afya Ummy Mwalimu anatarajiwa kuzindua Ripoti ya Viashiria Muhimu vya Utafiti wa Afya ya Uzazi na mtoto na viashiria vya Malaria wa mwaka 2022.

Ripoti hiyo inatarajiwa kuzinduliwa kesho Januari 7,2023 katika viwanja vya ofisi ya Taifa ya Takwimu(NBS)jijini Dodoma.

Hayo yamesemwa jijini hapa leo na Meneja wa Takwimu za Jamii,Sylvia Meku wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu ujio wa uzinduzi huo ambapo ametaja lengo kuu la utafiti huo ni kupata taarifa za sasa za afya na takwimu zinazohusiana na masuala ya afya ili kusaidia kuboresha sera katika ajenda ya maendeleo ya kitaifa,kikanda na kimataifa.

Lengo lingine ni kupata takwimu zitakazowezesha kupima viashiria vya malengo ya maendeleo ya kitaifa kama vile Dira ya maendeleo ya Tanzania 2025,Dira ya Maendeleo ya Zanzibar 2050,Mpango wa Taifa wa Tatu wa Maendeleo wa Miaka Mitano(FYDP III 2021/22-2025/26),mpango wa maendeleo wa Zanzibar wa mwaka 2021/22 hadi 2025/26,Dira ya Jumuiya ya Afrika Mashariki 2050(EAC 2050)Ajenda ya Maendeleo ya Afrika 2063(ADA 2063)na Ajenda ya Kimataifa ya 2030 kuhusu malengo ya maendeleo endelevu(SDGs 2030)na kutathmini hatua iliyofikiwa katika kuboresha hali ya maisha ya watu nchini.

“Utafiti huu ulifanyika kwakutumia njia ya sampuli wakilishi kuwakilisha nchi nzima yaani Tanzania Bara na Zanzibar ambapo jumla ya maeneo ya kuhesabia watu 629 yalichaguliwa kuwakilisha maeneo mengine,

“Kati ya maeneo hayo,maeneno ya kuhesabia wa 211 yalikuwa ni ya Mijini na 418 ya Vijijini ambapo kwa kila eneo la kuhesabia watu,kaya 26 zilichaguliwa kitalaamu kuwezesha upatikanaji wa sampuli ya kaya wakilishi 16,354 nchini,”amesema Meku.

Ameeleza kuwa utafiti huo ulifanywa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu(NBS),Ofisi ya ya Mtakwimu Mkuu wa serikali Zanzibar(OCGS)na Wizara ya Afya Bara na Zanzibar kwakushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu,Ofisi ya Rais,Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI),Wizara ya Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wanawake na Makundi Maalum,Taasisi ya chakula na lishe Tanzania,mpango wa Taifa wa kudhibiti Malaria,Chuo cha Takwimu Mashariki mwa Afrika,Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine na Chuo Kikuu cha Dodoma.