March 28, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waziri Ummy apiga marufuku matumizi ya shisha

Zena Mohamed,TimesMajiraOline,Dodoma.

WAZIRI wa Afya Ummy Mwalimu amepiga  marufuku matumizi ya kilevi aina ya shisha na kusema matatizo yatokanayo na bidhaa za tumbaku ni makubwa kiasi kinacho sababisha vifo kwa karibu nusu ya watumiaji wake na zaidi ya watu takribani milioni 8 Kila mwaka duniani kwa sababu ya matumizi ya tumbaku.

Ameeleza milioni Saba ya vifo hivyo hutokana na matumizi ya Moja kwa moja wakati milioni 1.2 ni kutokana na utumiaji wa bidhaa za tumbaku usio wa moja kwa moja .

Waziri Ummy amesema hayo Jijini hapa leo wakati akizungumza na Waandishi wa habari kuhusu maadhimisho ya siku ya kutotumia tumbaku duniani na kubainisha kuwa asilimia kubwa ya watu walioko kwenye nchi zinazoendelea ndiyo huathirika zaidi ikilinganishwa na nchi zilizoendelea.

Amesema hali hiyo imekuwa ikileta changamoto kwenye sekta ya afya na kusababisha rasilimali ndogo iliyopo kutotosha kukidhi mahitaji ya huduma kwa wagonjwa kwa kushindwa kuwahudumia ipasavyo na hivyo kusababisha vifo ambavyo vingeweza kuepukika .

“Mbali na madhara ya kiafya yatokanayo Moja kwa moja na matumizi ya tumbaku ,pia kuna uchafuzi wa mazingira ,tuchukulie mfano sigara takribani 65 ya wavutaji sigara hutupa vishungi vyake barabarani,kwenye fukwe za bahati na maziwa,”amesema.

Ameeleza, takribani tani milioni 25 za taka zitokanazo na tumbaku huzalishwa kila mwaka kutokana na mzunguko wa maisha ya tumbaku na kwamba Kuna zaidi ya kemikali 7000 zinatolewa kwenye mazingira kutokana na matumizi ya sigara huku 70 kati ya hizo zimethibitika kuwa na uwezo wa kusababisha saratani.

“Tanzania inawajibika kuandaa mikakati mbalimbali ya kudhibiti na kupunguza matumizi ya bidhaa za tumbaku ili kuziepusha jamii dhidi ya madhara ya bidhaa hizo ambapo TMDA imeanza kazi ya udhibiti wa bidhaa kwa kusajili bidhaa za tumbaku,kufanya ukaguzi na uchunguzi wa kimaabara na kuelimisha Umma,”amesema

Ametaja mikakati mingine  kuwa ni kuhakikisha majengo yote ya Umma yanatenga maeneo maalum ya utaji na yasiyo ya uvutaji ili kulinda afya ya jamii,kuchangia kulinda mazingira kwa kupunguza uchafuzi
na kusimamia utekelezaji wa bidhaa za tumbaku zisizofaa kwa matumizi.

Waziri huyo pia alisema Ili kufikia lengo la kutokomeza athari zote za kiafya zinzosababishwa na tumbaku,Tanzania itaendelea kushiriki katika jitihada za Kitaifa na kimataifa za kudhibiti matumizi ya baadhi ya bidhaa za tumbaku kama vile shisha ,ugoro na sigara za kielekroniki.

Kila mwaka ifikapo 31, Mei,2022 nchi zote duniani kwa kushirikiana na Shirika la afya duniani huadhimisha siku hii Kwa lengo la kuelimisha jamii madhara ya kiafya na athari za mazingira yatokanayo na bidhaa za tumbaku na hatimaye kupunguza na kutokomeza matumizi ya tumbaku Ili kulinda afya ya jamii na mazingira.