March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waziri Mulamula aagana na Balozi wa Ubelgiji nchini

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula ameagana na Balozi wa Ubelgiji nchini Mhe. Peter Van Acker ambaye amemaliza muda wake wa uwakilishi hapa nchini.

Akizungumza na Mhe. Balozi Peter walipokutana katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam, Waziri Mulamula amesema Tanzania na Ubelgiji zimekuwa na uhusiano wa karibu tangu nchi hiyo ilipofungua Ubalozi wake hapa nchini mwaka 1980.

Waziri Mulamula ampongeza Mhe. Balozi kwa kumaliza utumishi wake nchini na kuacha uhusiano kati ya Tanzania na Ubelgiji ukiwa imara.

Balozi Mulamula amesema pamoja na kwamba Balozi Peter anaondoka nchini amemhakikishia kuwa kundi la wafanyabiashara kutoka Ubelgiji litakuja nchini mwaka huu ikiwa ni mwendelezo wa kukuza ushirikiano wa kibiashara na uwekezaji.

Kwa upande wake, Balozi wa Ubelgiji nchini, Mhe. Peter Van Acker ameongelea kuridhishwa kwake na uhusiano uliopo baina ya Ubelgiji na Tanzania na kuahidi kuwa balozi mwema wa Tanzania.