May 16, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waziri Mkuu Majaliwa akagua ujenzi soko la machinga,alipongeza jiji la Dodoma kwa mradi huo

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma

WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amefanya ziara ya kukagua ujenzi wa soko la machinga linalojengwa katika eneo la Bahi Road (uwanja wa Ndega) jijini Dodoma kwa kutumia mapato yake ya ndani kwa lengo la kuwaleta pamoja wafanyabiashara ndogo ndogo na kuwawezesha kufanya kazi zao katika mazingira rafiki.

Akizungumza mara baada ya kukagua ujenzi wa soko hilo ambalo amesema mara baada ya kukamilika litakuwa ndio soko bora la machinga kuliko masoko ambayo yapo katika mikoa mingine.

Aidha katika ziara hiyo ya Waziri Mkuu ,waliakwa wakuu wa wilaya na wakurugenzi kutoka wilaya nyingine za mkoa wa Dodoma ili kwenda kujifunza na kuona jinsi Jiji la Dodoma linavyotumia mapato yake ya ndani katika kuwaletea wananchi maendeleo huku akiwaagiza wakuu wa mikoa,wakurugenzi na wakuu wa wilaya kote nchini kuiga mfano wa jiji la Dodoma kupitia mradi huo wa ujenzi wa soko la wamachinga.

Aidha amewataka wakuu wa Wilaya na wakurugenzi wa mkoa wa Dodoma kwenda kuwauganisha pamoja wafanyabiashara wote ili iwe rahisi kupatiwa mitaji na kuweza kusaidiwa katika shida nyingine.

“Kwa namna nilivyoona na maelezo ya kazi inavyoendelea ,soko hili linaweza kuwa la mfano nchi nzima …,Rais wetu Samia Suluhu Hassan ana dhamira njema ya kuhakikisha watanzania wanaingia na kufanya biashara kwenye mazingira mazuri bila kujali ana mtaji wa kiasi gani .”amesema Majaliwa

Ametumia nafasi hiyo kulipongeza jiji la Dodoma kwa kazi hiyo kwani baada ya kukamilika wamachinga watafanya kazi zao katika mazingira ambayo hanaya usumbufu kwao wa kuhamahama haswa kipindi cha mvua.

“Hii ni kazi ya kupongezwa ,maana hapa kutakuwa hakuna jua wala mvua ,sasa hivi ,mnaweza msielewe ninachokizungumza ila mtakuikumbuka kauli hii hapo baadaye.”amesisitiza

Hata hivyo a,esema eneo hilo bado halitatosha kwa wamachinga wote huku akiliagiza jiji la Dodoma kuangalia maeneo mengine ambayo ni rafiki kwa wafanyabiashara hao wadogo ili wajenge masoko ,mengine na kusogeza huduma hizo katika maeneo mengi.

” Sasa wakuu wa wilaya,wakurugenzi wa wilaya nyingine za mkoa wa Dodoma nanyi nendeni mkawaunganishe kwenye vikundi wafanyabishara wadogo na wenye biashara zinazofanana ili waweze kusaidika kiurahisi.”

Waziri Mkuu Majaliwa amewataka wafanyabiashara hao wadogio watakaokosa nafasi katika eneo hilo wasikate tama kwani bado Serikali inafikiriwa kujengwa masoko kama hilo katika  maeneo mengine .

Kwa upande wake Waziri kutoka Ofisi ya Rais Tawala za mikoa na Serikali za Mitaa TAMISEMI Innocent Bashungwa amelipongeza jiji la Dodoma kwa kuwa wabunifu kwa kuweza kutengeneza soko hilo la wazi kwa wafanyabiashara wadogo wadogo Maarufu kama machinga .

” Wakuu wa mikoa mingine igeni mfano huu mzuru wa mkoa wa Dodoma  katika ujenzi huu kueni wabunifu kulingana na maeneo lenu au mikoa yenu mnayofanyia kazi,” amesema Bashungwa

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa (Mwenye tai nyekundu)akitembelea soko la machinga Bahiroad jijini Dodoma ,kulia kwake ni mkuu wa mkoa wa Dodoma Anthony Mtaka,pamoja na viongozi wengine wakiwemo Mawziri

Waziri kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi Vijana Ajira na Wenye Ulemavu Profesa Joyce  Ndalichako amesema machinga wa mkoa wa Dodoma hawatakuwa na shida tena kwani sasa wanaweza kufanya kazi katika mazingira mazuri licha ya hapo awali jambo hilo kuonekana kama ndoto.

” Vijana kumbukeni Rais wa awamu ya sita onaongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan imewajali wajasiriamali  hivyo niwaombe vijana msichague kazi kwani eneo hilo limejengwa kwaajili ya machinga tuchangamkie fursa katika eneo hili,” amesema Waziri Ndalichako.

Naye Mkuu wa mkoa wa Dodoma Anthony Mtaka amesema,baada ya mradi huo kukamilika hakuna wafanyabiashara wadogo (wamachinga) watakaobaki barabarani kwa ajili ya kufanya biashara zao.

Mkurugenzi wa jiji la Dodoma Joseph Mafuru akitoa taarifa fupi ya ujenzi wa soko la machinga

Awali akisoma taarifa ya ujenzi huo Mkurugenzi wa jiji la Dodoma Joseph Mafuru amesema jiji la Dodoma linafanya juhudi kuhakikisha eneo hilo linakamilika kwa wakati ambapo kwa ujenzi wa awali watachukuliwa wajasiriamali 2000 kuweza kufanya biashara katika eneo hilo.

Pia amesema kukamilika kwa soko hilo jiji la Dodoma litaweza kukusanya Shilingi Bilion 1 kwa mwaka kutokana na tozo mbalimbali zotakazotozwa katika katika eneo hilo.